Wednesday, December 17, 2014

WABONGO WAMFUTA MACHOZI MISS TZ

SIKU chache baada ya kupatikana kwa mshindi wa Shindano la Miss World 2014, imethibitika kuwa Wabongo walimfuta machozi mshiriki wao, Happiness Watimanywa kwa kumpigia kura nyingi zilizosababisha kuingia hatua ya Kumi Bora ya Chaguo la Watu (People’s Choice).
Happiness Watimanywa akiwa na mrembo wa dunia Rolene Strauss wa Afrika Kusini.
Kwenye shindano hilo lililofanyika Jumapili usiku huko London nchini Uingereza, ambalo Rolene Strauss wa Afrika Kusini aliibuka kidedea, watu wengi hawakushangazwa na matokeo hayo.
Wakizungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti, wadau mbalimbali wa masuala ya urembo walimtaka Miss huyo kujipongeza kwa hatua aliyofikia kwani kama suala la kupiga kura, wengi walijitolea na ndizo zilizosababisha aingie katika Kumi Bora ya People’s Choice.
“Asijali, tuko nyuma yake na tunampongeza kwa hatua aliyofikia. Mashindano ya urembo katika ngazi ya dunia yana changamoto nyingi hivyo kwa pamoja tunajipongeza maana safari hii Wabongo wameamka na kujitoa sana kupiga kura,” alisema mmoja wa wadau ambaye hakutaka jina lake lichorwe gazetini.