Monday, January 19, 2015

KWAKO MWANAUME FAHAMU JINSI YA KUWA BABA MZURI KATIKA FAMILIA . HIZI HAPA NGUZO TANO

“Kwani nilikosea wapi?” Swali hilo lilimsumbua
sana Michael, * anayeishi Afrika Kusini. Ingawa
alijitahidi sana kuwa baba mzuri, kila mara
alipofikiria kuhusu mwana wake mwenye umri wa
miaka 19 aliyeasi, alijiuliza ikiwa alifanya yote
aliyoweza ili kuwa mzazi mzuri.
Kwa upande mwingine, inaonekana kwamba Terry,
anayeishi Hispania amefaulu kuwa baba mzuri.
Andrew, mwana wake, anasema hivi: “Baadhi ya
mambo ninayokumbuka kuhusu maisha yangu ya
utotoni ni baba yangu akinisomea, akicheza nami,
na tukienda matembezi pamoja ili tu mimi na yeye
tuwe pamoja. Alinifanya nifurahie kujifunza.”
Ni kweli kwamba si rahisi kuwa baba mzuri. Lakini
kuna kanuni za msingi ambazo zinaweza
kukusaidia. Akina baba wengi wamegundua
kwamba wao na familia zao hunufaika sana
wanapofuata hekima iliyo katika Biblia. Acheni
tuchunguze baadhi ya mashauri yanayopatikana
katika Biblia ambayo yanaweza kuwasaidia akina
baba.
1. Tenga Wakati wa Kuwa
Pamoja na Familia Yako
Wewe baba unaonyeshaje kwamba watoto wako ni
muhimu? Bila shaka kuna mambo mengi ambayo
wewe huwafanyia watoto wako, kutia ndani
kujinyima mambo fulani ili kuwapa chakula na
makao yanayofaa. Hungefanya mambo hayo ikiwa
watoto wako si muhimu kwako. Hata hivyo, ikiwa
hutumii wakati wa kutosha pamoja na watoto
wako, huenda wakaona kwamba kazi yako, marafiki
wako, au mambo unayopenda kufanya ni muhimu
kuliko wao.
Baba anapaswa kuanza kutenga wakati wa kuwa
pamoja na watoto wake wanapokuwa na umri
gani? Mama huanza kuwa na uhusiano na mtoto
wake anapokuwa bado tumboni. Majuma 16 hivi
baada ya mimba kutungwa, mtoto aliye tumboni
anaweza kusikia. Wakati huo, baba pia anaweza
kuanza kujenga uhusiano wa pekee pamoja na
mtoto wake ambaye bado hajazaliwa. Anaweza
kusikiliza mapigo ya moyo wa mtoto, kumsikia
akicheza, kuzungumza naye, na kumwimbia.
Kanuni ya Biblia: Katika nyakati za Biblia, wanaume
walipaswa kuwafundisha watoto wao. Akina baba
walitiwa moyo watumie wakati na watoto wao kwa
ukawaida, kama inavyoonyeshwa na Biblia kwenye
andiko la Kumbukumbu la Torati 6:6, 7 , linalosema
hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima
yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana
wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako
na unapotembea barabarani na unapolala na
unapoamka.”
2. Baba Wazuri Wanajua Jinsi
ya Kuwasiliana
Ili uwasiliane kwa njia
nzuri na watoto wako,
lazima uwe msikilizaji
mzuri. Unapaswa
kusitawisha uwezo wa
kusikiliza kwa utulivu.
Ikiwa watoto wako
watahisi kwamba
utakasirika na
kuwahukumu, hawatajihisi
huru kukueleza yaliyo moyoni. Lakini ukisikiliza
kwa utulivu, unawaonyesha kwamba unawajali
kikweli. Ukifanya hivyo, yaelekea watakuambia
mawazo na hisia zao za ndani.
Kanuni ya Biblia: Hekima inayopatikana katika
Biblia imethibitika kuwa yenye manufaa katika
sehemu nyingi za maisha. Kwa mfano, Biblia
inasema: “Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu
kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa
ghadhabu.” (Yakobo 1:19 ) Akina baba wanaofuata
kanuni hiyo ya Biblia hufanikiwa kuwasiliana na
watoto wao kwa njia nzuri.
3. Toa Nidhamu kwa Upendo
na Uwapongeze
Hata wakati ambapo unahisi umekasirika, nidhamu
unayotoa inapaswa kuonyesha kwamba unampenda
mtoto na unajali maisha yake ya siku zijazo.
Nidhamu inatia ndani kumshauri, kumrekebisha,
kumwelimisha, na kumwadhibu inapohitajika.
Isitoshe, nidhamu inakuwa na matokeo zaidi ikiwa
baba ana zoea la kuwapongeza watoto wake.
Methali ya kale inasema hivi: “Neno linalosemwa
wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya
dhahabu kwenye chombo cha fedha
kilichopambwa.” (Methali 25:11 ) Pongezi
humsaidia mtoto kukuza sifa nzuri. Watoto
hujiheshimu wanapoona kwamba wazazi wao
wanawajali na kuwathamini. Baba anayetumia kila
fursa kuwapongeza watoto wake atawasaidia
wajiheshimu na kuwachochea kutenda yaliyo sawa.
Kanuni ya Biblia: “Enyi akina baba, msiwe
mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike
moyo.” — Wakolosai 3:21 .
4. Mpende na Kumheshimu
Mke Wako
Jinsi baba
anavyomtendea mke
wake kutakuwa na
uvutano mzuri au mbaya
kwa watoto wake.
Wataalamu wa ukuzi wa
mtoto wanasema hivi: “Mojawapo ya mambo bora
ambayo baba anaweza kuwafanyia watoto wake ni
kumheshimu mama yao. . . . Baba na mama
wanaoheshimiana na kuacha watoto wao waone
jambo hilo huwafanya watoto wawe na furaha na
wahisi wanapendwa.”— The Importance of Fathers in
the Healthy Development of Children. *
Kanuni ya Biblia: “Enyi waume, endeleeni
kuwapenda wake zenu, . . . Kila mtu mmoja-
mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake
kama vile anavyojipenda mwenyewe.” — Waefeso
5:25, 33 .
5. Tumia Hekima Kutoka kwa
Mungu
Akina baba wanaompenda Mungu kutoka moyoni
wanaweza kuwapa watoto wao urithi wenye
thamani, yaani, uhusiano wa karibu pamoja na
Baba yao wa mbinguni.
Baada ya kufanya kazi
ngumu ya kuwalea
watoto wake sita kwa
miaka mingi, Antonio,
ambaye ni Shahidi wa
Yehova alipokea barua hii
kutoka kwa mmoja wa binti zake: “Baba mpendwa,
nilitaka kukushukuru kwa kunilea na kunifundisha
kumpenda Yehova Mungu, kujipenda mwenyewe,
na kumpenda jirani yangu, yaani, ulinisaidia kuwa
mtu mwenye usawaziko. Ulinionyesha kwamba
unampenda Yehova na kwamba unanijali. Asante
Baba kwa kumtanguliza Yehova maishani mwako
na kuwaona watoto wako kuwa zawadi kutoka kwa
Mungu!”
Kanuni ya Biblia: “Lazima umpende Yehova Mungu
wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote
na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya
ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako.”—
Kumbukumbu la Torati 6:5, 6.
Ni wazi kwamba kuwa baba kunahusisha mengi
zaidi ya mambo hayo matano, na hata ukijitahidi
kiasi gani, hutakuwa baba mkamilifu. Lakini
ukijitahidi kutumia kanuni hizo kwa upendo na
usawaziko, unaweza kuwa baba mzuri. *