Friday, April 3, 2015

DIAMOND, HAYA NI YA KITOTO MSHIKAJI!

NIANZE kwa kutoa pole kwa wadau wote wa muziki wa kizazi kipya, kwa kuondokewa na mdau Abdul Bonge, muanzilishi wa Kundi la Tip Top Connection, wale vijana wenye maskani yao pale Manzese.
Bonge ametutoka katika wakati ambao Bongo Fleva ndiyo ilikuwa inamhitaji zaidi, kwani hakuna ubishi kwamba muziki huu sasa unalazimisha njia kuelekea nje ya nchi na hawa ndiyo walikuwa wawezeshaji wakuu wa jambo hili. Mungu ampe mapumziko mema peponi na tumuahidi tu kuwa nasi tupo njiani, tutakutana naye muda na wakati wowote kuanzia sasa!
Baada ya pole hiyo, kwa wasanii, wadau na jamii yote, sasa nirejee kwenye mada yangu ambayo nazungumza na staa wa Bongo Fleva aliye katika levo za juu kabisa, Diamond Platnumz.
Hivi karibuni kulikuwa na habari zilizosema kuwa msanii huyo amehamia katika nyumba yake ya bei mbaya aliyoijenga huko Madale, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam. Kabla ya kuhamia, kama walivyo vijana wengi wa sasa, ‘alitupia’ picha kadhaa katika akaunti yake kwenye mtandao wa Instagram akionyesha sehemu mbalimbali za nyumba hiyo ya kisasa.
Alionyesha bwawa la kuogelea, samani zilizopo sebuleni na jikoni kwake sambamba na vitu vingine vilivyoendana na jumba lake hilo. Lakini katika hali ya kushangaza, siku chache baadaye alisikika akisema kutokana na ukubwa na thamani ya nyumba yake, vinamfanya ahofie maisha yake, hasa nyakati za usiku anaporejea kutoka kazini au matembezini (Wasanii mara nyingi hufanya kazi usiku).
Kwanza nimpongeze sana Diamond kwa kufanikiwa kumalizia nyumba yake maana vijana wengi wa umri wake, bado wanaishi kwa wazazi wao. Lakini wakati nikimpongeza, napenda pia kumshauri kuwa hivi sasa ameshakua mkubwa, siyo tu kiumri, bali hata kiakili, kiasi kwamba anapaswa kuacha kufanya baadhi ya mambo ambayo kimsingi, yanapishana naye.
Hatari anayoihisi kule nyumbani kwake alikojenga, ameitengeneza mwenyewe. Ujana na ukisasa, unamfanya kuweka picha za baadhi ya vitu vilivyomo ndani ya nyumba yake, jambo ambalo siyo baya, lakini unapoishi na jamii iliyokata tamaa kama yetu, siyo jambo zuri.
Nchi yetu ina vijana wengi wasio na ajira, ambao wamekosa fursa na bahati mbaya, wengi wao hawana elimu ya kutosha. Matokeo yake wanaishi kwa kubangaiza ilimradi siku zinakwenda. Wakati Diamond ana uwezo wa kujenga nyumba yenye thamani ya shilingi milioni 400, wenzake wengi hawana hata uhakika wa mlo wa siku.
Aina ya maisha ya Diamond, yanashawishi watu kudhani ni tajiri sana, mwenye uwezo mkubwa kimaisha na hivyo ni kijana anayenuka fedha. Kama nilivyosema, anaweza kuwa ni shabiki wa wengi, lakini unapofikiria kuhusu tabu za maisha, watu hawaoni hatari kumdhuru ilimradi kama wana uhakika kuwa watapata kitu cha kuwapunguzia ukali wa maisha.
Nadhani huu ni wakati wa Diamond kupunguza maisha ya video. Ni haki yake kuamua chochote kinachomhusu, lakini busara haishawishi mtu kutangaza unachomiliki pasipo sababu za msingi. Binafsi ninawajua wasanii wengi ambao ‘wako vizuri’ kimaisha, lakini huwezi kuwadhania ukiwaona.
Yapo baadhi ya mambo tunayafanya kwa sababu ya umri, ambayo kadiri tunavyokua hatuwezi kufanya. Wabongo hawajui kuwa unaweza kuwa na nyumba kubwa, lakini usiwe na fedha ndani, watakuja na mapanga yao kulazimisha uwape fedha, wasipopata utaambulia majeraha.
Ni kweli hata mastaa wa Ulaya wanaanika wanachomiliki, lakini tambua kuwa ipo tofauti kubwa kati yetu. Wewe bado ni kijana mwenye ndoto nyingi, acha matangazo, timiza ndoto zako!