Wednesday, April 22, 2015

WASTARA: NINA JINAMIZI LA AJALI!

Waandishi wetu
BAADA ya kunusurika kifo katika ajali ya gari, ambayo mwenyewe amesema ni ya tisa tokea ajitambue, muigizaji nyota Wastara Juma, amesema anaamini ana jinamizi la ajali linalomuandama, Risasi Jumatano lina mkasa kamili.
Wastara akiwa na majeraha usoni baada ya kupata ajali ya gari maeneo ya Tabata.
Wastara, akiwa katika gari lililokuwa likiendeshwa na msanii mwenzake, Bond Bin Suleiman majira ya saa nne usiku maeneo ya Tabata, walipata ajali hiyo baada ya gari lisilofahamika, kukatiza kabla mbele yao na dereva alipofunga breki ghafla, muigizaji huyo ambaye hakuwa amevaa mkanda wakati huo, alitoka kwenye kiti na kwenda kujigonga kwa nguvu kwenye ‘dashboard’.
Kitendo hicho cha kujigonga kwa nguvu kilisababisha kujichana sehemu ya juu ya jicho lake la kulia, kitu ambacho kilimpa maumivu makali. Alipokwenda kupata matibabu katika zahanati ya Kilimanjaro, alihudumiwa na kuruhusiwa kurudi nyumbani.
Muigizaji nyota Wastara Juma.
Akizungumzia ajali hiyo, Wastara, mjane wa nyota wa zamani wa filamu, Juma Kilowoko ‘Sajuki’, alisema kwa jinsi zinavyomuandama mara kwa mara tokea alipopata ajali ya kwanza akiwa na umri wa miaka kumi, anaamini ana jinamizi.
“Si bure, kutakuwa na kitu tu kisicho cha kawaida kwangu, lakini naamini Mungu yupo upande wangu, maana ajali hizi zote ni mbaya ambazo ningeweza kabisa kupoteza uhai,” alisema muigizaji huyo.