Saturday, June 13, 2015

MAMA AMCHOMA MOTO MTOTO MIAKA 7

Saimeni Mgalula, Mbeya
Ukatili kila kona! Mwanamke aliyetajwa kwa jina la mama Joy amechezea kipigo ‘hevi’ kutoka kwa wananchi wenye hasira kali akidaiwa kumchoma moto mikononi mtoto anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka saba ambaye jina halikupatikana kwa madai ya kumuibia shilingi elfu ishirini.
Mtoto huyo akiugulia maumivu baada ya kuchomwa moto na mamaa'ke.
Tukio hilo la kinyama ambalo ni sehemu ya matukio ya mateso kwa watoto yanayotokea kila kukicha maeneo mbalimbali nchini, lilijiri juzikati katika Mtaa wa Nello Kata ya Kaloleni wilayani Momba mkoani hapa majira ya saa 11:20 jioni.
Wakizungumzia tukio hilo, baadhi ya mashuhuda walisema kuwa mtoto huyo alikuwa akiishi katika mazingira magumu almaarufu kwa jina la chokoraa hivyo hana makazi maalum.
Walifunguka kuwa mara baada ya kuwa na maisha hayo, ilibidi mama Joy amuombe aishi naye ambapo mtoto huyo alikubali na kuacha kulala nje ya nyumba na udokozi kwa kuwa alikuwa anapata chakula.
Kwa mujibu wa mashuhuda hao, walisikia kelele za mtoto huyo akilia kwa sauti na walipotoka kumwangalia ndipo wakakuta ameungua mikono na alipoulizwa kulikoni alisema kuwa mama Joy ndiye aliyemchoma akimsingizia kuwa ameiba kiasi hicho cha fedha.
Walidai kwamba, baada ya kusikia hivyo, baadhi ya wananchi wenye hasira kali walianza kumbonda mama Joy huku wakimkokota kuelekea Kituo cha Polisi Tunduma ili sheria ichukue mkondo wake.
Hadi gazeti hili ‘linaanua matanga’ eneo la tukio mama huyo alikuwa ameshikiliwa polisi huku mtoto huyo akipelekwa hospitalini kwa matibabu.