Monday, July 6, 2015

TAHADHARI.. WANAUME MNAOVAA SURUALI MODO HATARINI KUITWA KAKA NA WAPENZI WENU...SOMA HAPA UJUE MADHARA YAKE

Bantaco Boys-one love-town_MG_3362 copy Pamoja na kuonekana kuwa ni fasheni (mtindo) inayowapendeza wanawake wengi na inayopata umaarufu zaidi kwa vijana wengi nchini,  wakiwemo wasanii,   ukweli ni kuwa suruali za jeans na zinazobana maarufu kama, ‘skinny jeans’…  ni bomu linaloleta madhara taratibu.
Uchunguzi wa kitaalam umebainisha kuwa suruali za kubana hasa za jeans zinasababisha maradhi mbalimbali ikiwemo kuharibika kwa mishipa ya fahamu, fangasi sehemu za siri na kupungua kwa nguvu za kiume.
Hii ni kwa sababu zinaibana mishipa inayotembeza damu mwilini  hasa katika mapaja, kibofu cha mkojo na korodani hivyo kushindwa kusambaza damu katika baadhi ya maeneo.
 Baadhi ya maeneo ambayo huathirika zaidi ni mapaja kwa wanawake, kibofu cha mkojo kwa wanaume, nguvu za kiume na kufa ganzi kwa miguu kwa wanawake,
Wataalamu wa afya wanasema kuwa unapovaa suruali ya kubana sana, mishipa midogo midogo inayosafirisha damu ambayo hubanwa.
“Kwa kawaida damu husafiri kwa kasi kama maji hivyo misuli inapobanwa, damu hushindwa kusafiri na kusababisha neva za fahamu kufa au kuharibika,” anasema Dk Makgato Thabo wa Hospitali ya Milpark,  Afrika Kusini.
Kliniki ya Mayo inaeleza kuwa suruali za jeans zinazobana huiua  mishipa ya fahamu na kusababisha ugonjwa  wa mapaja kufa ganzi kwa kitaalamu unafahamika kama ‘Meralgia Paresthetica’, ambao husababishwa na kubanwa kwa neva.
Utafiti kuhusu madhara ya suruali hizi, umefanywa na Kampuni ya TENA ya nchini Uingereza inayofanya kampeni ya bidhaa salama kwa wanawake na wanaume.
 Ilibainika kuwa mamia ya watu wanaovaa suruali hizo hupata madhara baada ya muda  kutokana na kubanwa kwa neva na misuli ya kusafirisha damu.
“Wanaume wanapata matatizo makubwa ya kupungua kwa nguvu za kiume, wanawake mbali ya mapaja na miguu kufa ganzi, lakini wana hatari ya kupata fangasi kwenye sehemu zao za siri,” anasema daktari wa kampuni hiyo, Hillary Jones.
 Dk Jones anayefanya kazi katika kampuni ya TENA alieleza kuwa wanaume wanapata matatizo zaidi kwani huweza kuharibu mfumo wa mkojo na kupinda kwa korodani .
“Ushauri wangu kwa wanawake na wanaume ni kuacha nafasi kubwa katika maeneo nyeti. Hakikisha suruali na nguo ya ndani vinapata nafasi na wala usibanwe kwa namna yeyote,” anasema Dk Jones.
Anaongeza: “Hakuna ubishi wanaume wanaovaa mavazi ya kubana, wanaharibu afya zao; Tafadhali msitangulize mitindo kabla ya afya.”
Kupinda kwa korodani kunatokea pale suruali inayobana inapozuia mirija ya mbegu za kiume kutembea kwa uhuru.
Hivyo basi, mbegu hizo hushindwa kusafiri katika njia yake na kupita katika njia nyingine jambo ambalo husababisha kusimama kwa usambaaji wa damu.
 Pia, suruali za kubana huongeza msukumo katika kibofu cha mkojo jambo ambalo husababisha bacteria kuzaliana na kuingia katika mwili hivyo kusababisha kuathirika kwa mirija ya mkojo.
 Dk Jones anashauri watu kuvaa suruali za jeans za kubana lakini zinazovutika ili kujiondoa katika hatari inayowakabili.
Kwa upande wake, daktari bingwa wa magonjwa ya ndani ya mwili, Meshack Shimwela anasema ni jambo la kweli kuwa wanaume kuvaa nguo zinazobana huathiri  kuzalishwa kwa shahawa.
“Maeneo ya korodani yanahitaji nafasi, kule kubanwa kunasababisha mbegu za kiume zisizalishwe inavyotakiwa,” anasema
 Pia, anaeleza kuwa licha ya suruali za kubana wasichana wanaopenda kuvaa  nguo za ndani zinazobana sana, wanajiweka katika hatari ya kupata maradhi ya fangasi kwa sababu ya joto jingi.
Naye daktari bingwa wa masuala ya mfumo wa mkojo kwa wanaume na uzazi kwa wanawake, Dk Sydney Yongolo anasema korodani zinahitaji joto la kadri ili kufanya kazi vizuri na kuzalisha shahawa.
“inapotokea zikabanwa sana mishipa midogomidogo inayofanya kazi ya kusambaza damu na kuzalisha mbegu hushindwa kufanya kazi,” anasema Dk Yongolo.
 Anasema mwanaume yeyote anafahamu kuwa wakati wa baridi korodani hushuka kutafuta joto na wakati wa joto hupanda ili kutafuta joto la kadri.
Hivyo basi, endapo mwanaume amevaa suruali za kubana korodani hushindwa kupanda au kushuka kama kawaida yake.
“Ni kama yai la kuku, wakati wa kuatamiwa linahitaji joto la kadri kwa siku 21 ili kifaranga kizaliwe, hivyo ndivyo ilivyo kwa mbegu za kiume,” anasema Dk Yongolo
Dk Yongolo anaongeza kuwa si suruali pekee, bali hata nguo za ndani zinazobana husababisha madhara makubwa kwa wanaume na wanawake na ndicho chanzo cha ugumba.
“Maeneo hayo yanahitaji nafasi, kwa sababu joto likizidi au likipungua uzalishaji na mfumo wote hubadilika,”anasema
Dk Karen Boyle wa Hospitali ya Greater Baltimore, Uingereza anasema kwa bahati mbaya, tatizo hili huwa kubwa zaidi kwa wanawake wanaovaa suruali za jeans za kubana sambamba na viatu vyenye kisigino kirefu.
Anasema, wanawake wanaovaa viatu vyenye visigino virefu pamoja na suruali za kubana misuli yao hukaza, mishipa hushindwa kusafirisha damu na  hivyo kuwa katika hatari ya kupata maradhi ya kufa kwa ganzi kwa miguu na mapaja.
“Baada ya muda, wanapata misuli midogomidogo yenye rangi ya kijani na nyekundu au rangi ya kijani, jambo linaloonyesha usafirishaji duni wa damu katika maeneo hayo,” anasema Dk Boyle.
Source: Mwananchi