Wednesday, January 20, 2016

AZAM FC YAREJEA KILELENI LIGI KUU, MGAMBO WACHAPWA 2-1 MKWAKWANI

AZAM FC imerejea kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji Mgambo JKT Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga jioni ya leo.
Ushindi huo unaifanya Azam FC ifikishe pointi 39 baada ya kucheza mechi 15, ikiwazidi kwa pointi tatu mabingwa watetezi, Yanga SC ambao hata hivyo wana mechi moja mkononi na watacheza na Majimaji kesho Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Shomary Kapombe (kushoto) akikimbia kushangilia na Ame Ali 'Zungu' baada ya kufunga, huku kipa wa Mgambo, Said Lubawa akiwa ameketi chini

Shujaa wa Azam FC alikuwa ni beki wa kulia, Shomary Kapombe aliyefunga mabao yote mawili kipindi cha kwanza, baada ya Mgambo kutangulia kwa bao la Bolly Shaibu dakika ya 16.
Kapombe alifunga bao la kwanza dakika ya 22 akimalizia mpira uliotemwa na kipa Said Ludawa baada ya shuti la mshambuliaji John Raphael Bocco. 
Kapombe tena akapewa pasi nzuri na Nahodha Bocco kabla ya kuwahadaa mabeki wa Mgambo na kufumua shuti lililompita kipa Lubawa dakika ya 36.