Sunday, January 24, 2016

BAADA YA TAREHE YA UCHAGUZI ZANZIBAR KUTANGAZWA..CUF WATOA MSIMAMO WAO

Kufuatia tangazo jengine la kihuni lisilozingatia Katiba wala Sheria la Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) Jecha Salim Jecha kutangaza tarehe 20 Machi, 2016 kwamba ni siku ya kile anachokiita uchaguzi wa marudio Zanzibar, Chama Cha Wananchi (CUF) kimeitisha vikao vya juu vya kitaifa vya Chama ili kujadili suala hilo na kutoa msimamo rasmi wa Chama.
Kamati ya Utendaji ya Taifa itakutana Jumatano, tarehe 27 Januari, 2016 na kufuatiwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa litakalokutana Alkhamis, tarehe 28 Januari, 2016. Vikao hivyo vitafanyika Ofisi Kuu ya Chama, mjini Dar es Salaam.
Chama kinatoa wito na kuwanasihi Wazanzibari wote waliochoshwa na utawala wa kibabe na wa kidikteta wa CCM na ambao walikikataa chama hicho kwa kishindo tarehe 25 Oktoba, 2015 kuendelea kutunza amani na kuwa watulivu katika kipindi hiki kigumu na kusubiri maamuzi ya chama chao wanachokiamini.

HAKI SAWA KWA WOTE

ISMAIL JUSSA
KAIMU MKURUGENZI WA HABARI NA MAWASILIANO