Saturday, September 6, 2014

WASTARA afundishwa kuvaa vimini, kwenda klabu

WIKI iliyopita tuliishia pale mwigizaji Wastara Juma alipokuwa akimwelezea mchumba wake wa pili alivyokuwa hajatulia kiasi cha kumchanganya na wanawake watatu tofauti. Leo anaelezea alivyokutana na majanga mengine kwa mwanaume mwingine.
“Huyu mwanamke wa tatu baada ya kuondoka niliomba namba yake kwa mdogo wake huyo mchumba, nikampigia na kumuomba nionane naye. Bila hiyana alinikubalia, nilipoonana naye ndipo akanipasulia siri zote za yule mwanaume, iliniuma sana.
“Kutokana na ubishi wangu, nikawa kama siaminiamini, akaniambia kama siamini niende kuangalia albamu yake ambapo niliporudi kwao niliangalia albamu yake na kukuta picha akiwa na wanawake tofauti tena kimahaba, nilipotoka hapo sikurudi tena na aliponitafuta kwa simu nilimwambia simuhitaji tena.
Mwandishi: Baada ya kuachana na huyo mchumba ulimpata mwingine?
“Ndiyo nilikutana na mwanaume anaitwa Kushi ambaye hatukuchunguzana muda mrefu tukaoana, baada ya ndoa niligundua kwamba ni mlevi kupindukia, siyo mwaminifu na alikuwa mkorofi sana hivyo wiki moja baada ya ndoa tulipigana sana baa.
“Alikuwa akioa asubuhi na jioni kwani ndani ya ndoa yangu alioa wanawake watano na kuwaacha, alikuwa ni tajiri sana lakini alipenda starehe kupindukia hakuwa akinijali hata nguo ya ndani nilikosa nilikuwa navaa zilizochanika, nakumbuka nikiwa na ujauzito aliniambia maisha ni magumu niende nyumbani kwetu nirudi baada ya wiki mbili atakuwa ameshapata hela ya kodi ya nyumba.
“Wiki mbili nilizomuacha alioa mwanamke mwingine ambaye waliachana baada ya siku chache na kwenda Bagamoyo kwa mwanamke mwingine, maisha yake yakawa ndiyo hayo.
“Siwezi kumsahau huyu mwanaume na sitaki kumsikia kwa sababu aliniharibia dira nzima ya maisha yangu kwani kwake ndipo nilianza kuvaa suruali, kwenda klabu na baa wakati kabla ya hapo nilikuwa sivijui kabisa vitu hivi, alikuwa hataki niwe na marafiki akiona nina rafiki wa kike anatembea naye, kutokana na mateso hayo ilipofika mwaka 2001 tuliachana ikiwa ni baada ya kuishi kwa mwaka mmoja tu katika ndoa.
wastara
Mwandishi: Je nini kiliendelea baada ya kuachana na Kushi?
“Nilianza maisha yangu mwenyewe mpaka mwaka 2003 nikakutana na Msafiri Kondo (Solo Thang) ambaye tulikutana kwenye kazi baada ya tamasha ndiyo tukaanzisha uhusiano wa kimapenzi kwa muda mfupi nikapata ujauzito ndipo akarudi Kushi na kuomba msamaha.
“Alipoona nakataa kumsamehe akachunguza niko na nani akagundua ndipo alipomfuata Msafiri na kumtishia kwamba atamloga, nikamwambia Msafiri asihofu lakini akawa bado ana wasiwasi lakini naye sikumchunguza sana kabla kwani nilikuja kugundua kwamba alikuwa na mwanamke mwingine.
“Nilijifungua mtoto akiwa na siku tano Msafiri alisafiri na kwenda Ulaya ambako huko alioa na kuzaa watoto wawili hivyo akawa ananitumia matumizi ya mtoto mara mojamoja kwa hiyo kuanzia hapo nikawa nawalea wanangu wawili mwenyewe.
“Nilikaa mwenyewe na wanangu kuanzia mwaka 2004-2006 ambapo mwaka 2006 nilirudi rasmi kwenye sanaa ya filamu kwani mwanzoni nilifanya nikiwa shuleni.Wastara amezungumza vitu vingi kuhusu maisha yake. Usikose sehemu ya mwisho ya makala haya wiki ijayo!