Tuesday, November 4, 2014

MWANAMKE KIGOGO WA UNGA AHENYESHWA POLISI

SIKU chache baada ya Jeshi la Polisi Kitengo cha Kuzuia na Kupambana na Madawa ya Kulevya Tanzania kumkamata mfanyabiashara bilionea Mharami Mohamed Abdallah ‘Chonji’ mkazi wa Magomeni, Mtaa wa Kondoa jijini Dar akidaiwa kukutwa na unga, jeshi hilo linamhenyesha anayedaiwa kigogo mwingine wa unga ambaye ni mwanamke.
Christina Naphtali Kigaye mkazi wa Mikocheni anayehusishwa na biashara ya madawa ya kulevya.
Kamanda wa kitengo hicho, SACP Godfrey Nzowa, wiki iliyopita aliimbia Uwazi kwamba mwanamke huyo, Christina Naphtali Kigaye (pichani), mkazi wa Mikocheni, Dar alikuwa akitafutwa kwa muda mrefu na jeshi lake.
Kamanda Nzowa alisema, Christina amekuwa akitajwa na watu wengi wanaokamatwa na unga kuwa, yeye ndiye kigogo wa unga na amekuwa akiwabebesha mzigo na kuwatuma sokoni nje ya nchi.
Christina Naphtali Kigaye akiwa katika kituo cha polisi.
Kamanda Nzowa alisema siku ya tukio kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa  Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar, saa tatu asubuhi ya  Oktoba 29, mwaka huu, mtuhumiwa huyo akitokea nje ya nchi alinaswa baada kitengo chake kutonywa na watuhumiwa wengine ambao tayari wameshakamatwa lakini wakawa wanaijua ratiba yake.
“Pamoja na kwamba anadai kuwa anafanya biashara ya kuuza nguo na simu lakini hizo amejiegesha tu. Kwa mujibu wa watuhumiwa waliokamatwa na unga wamemtaja kwa asilimia kubwa kujihusisha na biashara hiyo haramu.
Baadhi ya madawa yaliyowahi kukamatwa.
“Kwa sasa upelelezi unaendelea dhidi yake na utakapokamilika hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa ikiwa na pamoja na kumpandisha mahakamani,” alisema Kamanda Nzowa.
Habari zaidi kutoka ndani ya jeshi la polisi zinadai kuwa mwanamke huyo alipelekwa makao makuu ya kitengo cha kuzuia madawa hayo Kilwa Road na kuhojiwa maswali mengi ambayo yalimtoa jasho.
“Alihojiwa kwa saa nyingi hadi akatokwa na jasho, maswali yalikuwa mazito,” alisema mtoa taarifa wetu.