Monday, November 3, 2014

UBAKAJI! BAUNSA AMSULUBU MSANII, NUSURA ABAKWE!

Ubakaji! Msanii wa muziki wa Kizazi Kipya kutoka Kundi la Fagio la Chuma ambaye pia aliwahi kuitumikia B-Band chini ya Banana Zorro, Hafsa Ally, amesulubiwa kisha kunusurika kubakwa na baunsa aliyemtaja kwa jina moja la Mahamoud.
Msanii wa muziki wa Kizazi Kipya kutoka Kundi la Fagio la Chuma, Hafsa Ally akielezea mkasa uliomsibu kwa waandishi wa Global.
Akizungumza na gazeti hili wikiendi iliyopita, Hafsa alisema tukio hilo lilijiri hivi karibuni, mishale ya saa 8:00 usiku alipokuwa akitokea Ukumbi wa Delux uliopo Sinza-Kijiweni, Dar akielekea nyumbani kwake maeneo ya Kijitonyama.
Hafsa alisema, akiwa kwenye Bajaj, ndipo akashtukia kuna bodaboda inawafukizia kwa nyuma.
“Nilipoangalia nyuma nikaiona pikipiki ambayo nilihisi kama inatufukuzia, lakini kabla sijakaa sawa nikashangaa kumuona Mahamoud ambaye namfahamu kama baunsa na dereva wa bodaboda.
Hafsa Ally akilia wakati anasimulia yaliyomsibu.
“Nilishangaa alipotufikia akiwa na mwenzake kwenye bodaboda alianza kunivuta nje huku Bajaj ikiwa kasi nikapata maumivu kwenye mbavu, michubuko mwilini na kunitegua bega,” alisema Hafsa na kuongeza:
“Baada ya kufanikiwa kuninyang’anya mkoba wangu alitaka kunibaka lakini nilipiga kelele kwa kushirikiana na dereva wa Bajaj niliyopanda ambapo wasamaria wema walijitokeza kunisaidia.
“Alipoona wananchi wamemzingira alitafuta upenyo na kukimbia ndipo nikaenda Kituo cha Polisi cha Urafiki (Dar) ambapo nilipewa fomu namba 3 (PF-3) kwa ajili ya kwenda kutibiwa.
“Nilikwenda kupata matibabu Hospitali ya Palestina (Sinza).
Hafsa Ally akionesha jeraha alilopata ubavuni wakati wa tukio.
“Baada ya kupatiwa matibabu nilimfungulia kesi yenye jalada namba URP/RB/8318/2014- JARIBIO LA UBAKAJI na tayari ametiwa mbaroni,” alisema Hafsa.