Tuesday, January 27, 2015

KISA SOMA HAPA:KIGOGO CCM AANGUA KILIO HADHARANI

Katibu wa Elimu, Malezi na Uchumi ambaaye pia ni Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wazazi wa CCM, Emmy Kiula kisikitikia jambo.

Machungu! Kigogo wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani hapa ambaye ni Katibu wa Elimu, Malezi na Uchumi na pia ni Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wazazi wa CCM, Emmy Kiula amejikuta akiangua kilio hadharani baada ya Mzee Mohamed Halfan (78) mwenye ulemavu kumlilia kuwa bwana shamba wa Kata ya Chazi (jina lipo), ameingiza mifugo yake kwenye shamba lake na kutafuna mazao yote.
Tukio hilo lilijiri kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kambi ya Walemavu wa Ukoma ya Chazi iliyopo Kata ya Chazi wilayani Mvomero mkoani hapa hivi karibuni ambapo Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa CCM Mkoa wa Morogoro, Mecktrdis Mdaku alifanya ziara ya ghafla katika kituo hicho.

Wakinamama wakimbembeleza Katibu Emmy Kiula asihuzunike. 
Baada ya kuwapa zawadi ya mbuzi, soda, unga sukari na mafuta ya kupikia walemavu hao waliomba kutoa kero zinazowakabili kwenye kituo hicho.
Baada ya ukimya wa kama dakika mbili, Mzee Halfan alijitoa muhanga na kupita mbele ya umati kisha kueleza kero yake ya bwana shamba huyo kuingiza mifugo yake kwenye mazao yake jambo lililomtia kigogo huyo uchungu na kujikuta akiangua kilio kweupe.
Licha ya kupelekwa pembeni na kubembelezwa, kigogo huyo aliendelea kulia hadi alipoamua kunyamaza.
“Hii siyo sawa kabisa hawa  wazee na ulemavu wao kiongozi unaingiza mifugo kwenye mazao yao, ningekuwa na mamlaka ningemfukuza kazi sasa hivi,” alisema mwenyekiti huyo na kushangiliwa na wazee hao huku akiomba serikali kumchukulia hatua bwana shamba huyo