Tuesday, September 29, 2015

KIPIMO CHAONESHA MAGUFULI ALAMA 6, LOWASSA ALAMA 9

Mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli.
WAKATI kampeni za kuwania Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zikizidi kupamba moto, vipimo vinaonesha mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli ana alama 6 na wa Ukawa, Edward Lowassa ana alama 9 katika mambo mbalimbali ya kikazi, Uwazi linachambua.
Uwazi lilianza kwa kuchimba kwenye upande wa mambo yaliyozua maswali mengi ambapo kipimo kinaonesha Magufuli, ambaye ni waziri wa ujenzi, alizua maswali kwenye uuzaji wa nyumba za serikali wakati wa uongozi wa serikali ya awamu ya tatu ya Rais Benjamin Mkapa na amesema atalitolea majibu.
Lowassa anatafunwa na vitu vitatu katika eneo hilo na ndilo eneo lenye kuharibu sifa ya mtu.
Cha kwanza ni ile kashfa ya Kampuni ya Kufua Umeme ya Richmond. Pili ni madai ya umiliki wa mali nyingi ambazo hazijaorodheshwa katika Tume ya Maadili na tatu ni madai kuwa, ni miongoni mwa Watanzania walioficha fedha Uswisi, mambo ambayo yanaweza kumpa wakati mgumu wa mbio zake za kwenda ikulu.
Katika utendaji wa kazi za kulitetea taifa, wagombea hao wamejikuta wakitoshana nguvu, kwani wote wamewahi kujitoa kulitetea taifa mara moja. Lowassa alivunja mkataba wa serikali na Kampuni ya kusambaza maji Dar, City Water baada ya kubaini hauna manufaa kwa nchi. Hapo alikuwa waziri wa maji, wakati Magufuli aliendesha oparesheni iliyofanikisha kukamatwa kwa meli iliyokuwa ikivua samaki katika kina kikubwa ndani ya Bahari ya Hindie eneo la Tanzania.
Katika utumishi wao serikalini, wagombea hao wanaopewa nafasi kubwa ya kuibuka kidedea katika uchaguzi huo, hawajafungana. Magufuli akitumika katika Wizara za Ujenzi na Uvuvi, wakati Lowassa akihudumu kama Waziri wa Maji, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (wakati wa Rais Ali Hassan Mwinyi), Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira na Umaskini) na baadaye waziri mkuu ambapo alijiuzulu kwa kashfa ya Richmond.
Katika kipengele cha kuwania urais, Lowassa anaonekana kumzidi Magufuli, kwani amewahi kuingia katika kinyang’anyiro hicho mara mbili, mwaka 1995 aliposhindwa na mwaka huu alipokatwa ndani ya CCM, lakini akaipata nafasi hiyo kutokea Ukawa.
Hii ni mara ya kwanza kwa Magufuli kujaribu na kupata nafasi ya kugombea nafasi hiyo ya juu kabisa kisiasa nchini huku akionesha kukubalika licha ya kwamba ni mara ya kwanza.Hii ndiyo tathmini ya Uwazi inayowapa alama hizo wagombea hao wawili ambao awali wote walikuwa miongoni mwa makada 43 wa CCM waliokuwa wameomba ridhaa ya kuteuliwa na chama hicho
-UWAZI