Saturday, May 24, 2014

POMBE SIO SUPU NA WALA SIO CHAI:KIJANA AFA KWA KUZIDISHA MITUNGI

MBALI ya jitihada mbalimbali zinazofanywa na makampuni ya kutengeneza pombe kutoa tahadhari kuwa unywaji wa pombe kupita kiasi ni hatari kwa afya, ‘janki’ Geoffrey Mlelwa (26), mkazi wa Ipogolo mjini hapa, amejikuta akiyakatisha maisha yake kwa kudaiwa kugida pombe kupindukia.
Mwili wq ‘janki’ Geoffrey Mlelwa ukiwa kwenye gari la polisi
 Tukio hilo la kusikitisha lilijiri juzikati ambapo kijana huyo alikuwa katika Soko Kuu la Manispaa ya Iringa akiwa na wenzake wakipiga ulabu kwa staili ya kuchanganya (kuchoma sindano) ndipo Geoffrey alipopitiliza na kusababisha apoteze uhai.
 Wakizungunza na mwanahabari wetu, baadhi ya mashuhuda walidai kuwa kijana huyo enzi za uhai wake alikuwa ni mtu wa kunywa pombe za kienyeji aina ya ulanzi na bangi ila siku hiyo alionekana mwenye ‘mihela’ hivyo kuachana na kunywa pombe aliyoizoea na kuanza kunywa pombe ya kisasa kama grants, viroba na kuchanganya na ulanzi ndani ya chupa moja.
 “Mbali ya ‘kuchanganya madawa’, kijana huyo hakula chakula chochote tangu alipoanza ‘kupiga vyombo’ na alipozidiwa, rafiki yake alimkokota na kumpeleka chumbani kwao (geto) kabla ya asubuhi kuamka na kumkuta amekufa,” alisema shuhuda mmoja kwa sharti la kutoandikwa jina gazetini.
 

Baba mzazi wa kijana huyo (pichani) mzee Guriano Mlelwa alithibitisha kutokea kwa kifo cha mwanaye na kuwa chanzo cha kifo hicho ni unywaji wa pombe kupita kiasi.
 Alisema kuwa kwa kawaida kijana wake anamtambua kama ni mlevi wa pombe na mtumiaji wa madawa ya kulevya na kuwa hata katika chumba chake walimkutana na chupa ambayo ndani yake ilikuwa imechanganywa pombe mbalimbali.
 Alisema anaamini kuwa mchanganyiko huo wa pombe na matumizi ya madawa ya kulevya ndivyo vilisababisha kifo hicho hivyo kuwashauri vijana kuachana na matumizi ya pombe kupita kiasi na madawa ya kulevya kwani wakiendelea kilichomuua mwenzao ndicho kitakachowaua.