Thursday, July 17, 2014

GARI LA MAREHEMU NGURUMO ALILOPEWA ZAWADI NA DIAMOND PLATNUM LAINGIZWA SOKONI KUUZWA

IKIWA takriban ni miezi minne kasoro tangu gwiji wa muziki Muhidin Mohamed Gurumo ‘Maalim Gurumo’ aiage dunia, gari aina ya Toyota Fun Cargo alilopewa kama zawadi na staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdu ‘Diamond’ limedaiwa kupigwa bei.
 
Gari alilokabidhiwa aliyekuwa gwiji wa muziki Muhidin Mohamed Gurumo ‘Maalim Gurumo’ ,  aina ya Toyota Fun Cargo.
 Chanzo makini kilicho karibu na familia kimepenyeza habari kuwa gari hilo lilizua utata baada ya kuwepo kwa mvutano baina ya baadhi ya ndugu na mke wa marehemu, Pili Nassoro ambapo walifikia hatua ya kufikishana polisi.
 “Kuna watoto wa marehemu walitaka kulipiga bei gari muda mchache tu baada ya kumaliza msiba ndipo utata ulipoanzia kwa sababu mjane wa marehemu hakukubali kwani inasemekana marehemu aliacha wosia kwamba pindi atakapofariki, kadi ya gari hiyo akabidhiwe mkewe,” kilisema chanzo hicho.
 
Maalim Gurumo akiwa ndani ya gari alilokabidhiwa na Diamond.
 Kikizidi kumwaga data chanzo hicho, kilidai kuwa Gurumo kabla hajafariki, alishajua tamaa ya baadhi ya ndugu zake hivyo aliamua kadi ya gari hiyo ibaki kwa meneja wa Diamond, Hamis Tale ‘Babtale’ ili hata akifa, apewe mkewe ambaye ndiye atakayekuwa na mamlaka na gari hilo.
“Marehemu alishawagundua baadhi ya ndugu wenye tamaa na mali hivyo akaona bora kadi hiyo ibaki kwa Babtale na kuacha wosia kwamba pindi akifa, akabidhiwe mkewe kama urithi wake,” kilisema chanzo hicho.

 
Maalim Gurumo akiwa na mke wake enzi za uhai wake.
 Alipotafutwa Babtale kuhusiana na kukabidhwa kadi ya gari hilo, alikiri kuwa nayo lakini akasisitiza kuwa ameshapokea maagizo kutoka kwa mjane wa marehemu kuwa liuzwe hivyo wateja wanaotaka kulinunua gari hilo wamwone yeye.
 “Kadi nilipewa kama meneja na msanii wangu (Diamond) nimtunzie kama maelekezo ambayo aliyatoa marehemu Gurumo hivyo akitokea mteja tunaliuza na fedha zote anachukua mjane wa marehemu,” alisema Babtale.
Diamond alimkabidhi marehemu gari hilo Agosti, mwaka jana katika Ukumbi wa Serena, Posta jijini Dar baada ya kuguswa na mchango mkubwa alioutoa Gurumo katika tasnia ya muziki nchini.