Tuesday, September 23, 2014

KUSHINDWA KUTENGA KWA SCOTLAND NA UINGEREZA KWAIFANYA CCM IKENUE MENO.

 
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana(kushoto) akisalimiana na wananchi baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Maili Moja, Kibaha, Mkoa wa Pwani mwishoni mwa wiki.(Picha na Bashir Nkoromo).


Kibaha. 
Kushindwa kujitenga kwa Scotland kutoka himaya ya ufalme wa Uingereza, kumetoa somo kwa wanasiasa kwamba hawana haki ya kuwafanyia uamuzi wananchi. 


Akitoa maoni yake kuhusiana na matokeo ya kura iliyopigwa wiki iliyopita nchini humo, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alisema sababu zilizoifanya Scotland kutaka kujitenga zinafanana na zile za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. 


Alisema ni vyema wananchi wakajifunza kuwa masuala kama hayo hayapaswi kujadiliwa kwa papara. 


“Waandishi wengi wamenipigia simu wakitaka kujua maoni yangu...mimi nasema kuwa suala hili limetufundisha kuwa jambo jema ni kubaki katika Muungano,” alisema Kinana alipohutubia mkutano wa hadhara katika Mji Mdogo wa Mlandizi, wilayani Kibaha Vijijini, Mkoa wa Pwani. 


Kinana alisema wakati wa kampeni, Waziri Mkuu wa Scotland, Alex Salmon aliwashawishi watu kupiga kura ya kujitoa. 


“Kulingana na kura za maoni watu wengi waliamini Scotland itajitoa katika himaya ya ufalme wa Uingereza, lakini matokeo ya kura yamekuwa tofauti. Hili ni funzo kwetu kuwa wanasiasa hawapaswi kuwa wasemaji wa wananchi au kuwafanyia uamuzi,” alisema na kuongeza kuwa wananchi wana haki ya kufanya uamuzi kwa mambo yanayohusu maisha yao. 


Alisema kila Muungano una matatizo na suluhu ni kuyajadili kwa umakini ili kuyapatia ufumbuzi wenye manufaa kwa wananchi. 


Kinana alisema matokeo ya kura hiyo yanaonyesha kuwa duniani kote watu wanapenda umoja kama ambavyo Watanzania wameudumisha. 


Aliwataka wanaozungumzia kuuvunja Muungano, kujifunza kutoka Scotland ambayo imekuwa mshirika na Uingereza kwa miaka 307 sasa. 


Awali, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema matokeo ya kura ya Scotland yamethibitisha kuwa Muungano wa hapa nchini utaendelea kudumu. “Kura hii imewakata kidomodomo wale wanaopigania kuuvunja Muungano wetu. Wameshaonyeshwa kuwa watu duniani kote wanapenda umoja,” alisema