Wednesday, December 24, 2014

PENNY UNATAKA MTOTO SAWA, UNAKUMBUKA MADUDU ULIYOYAFANYA NYUMA YA KUTOA MIMBA?

Kwako mtangazaji, Penniel Mungilwa ‘Penny’, mambo vipi? Mishemishe za mjini zinakwendaje? Umejiandaaje na Sikukuu ya X-Mas?


Binafsi mimi ni mzima wa afya, namshukuru Mungu hakuchi kunakucha. Naendelea na majukumu yangu ya kila siku maana kazi yangu mimi ni kama ya madaktari, haina cha sikukuu, nitalala uzeeni lakini sa hivi acha niendelee kusaka matukio na kuwajuza Watanzania.

Madhumuni ya kukukumbuka leo katika safu hii ya Barua Nzito ni kutaka kukukumbusha kwamba unapaswa kuwa makini katika nyendo zako. Maisha huwa hayajaribiwi, yakishapita ndiyo yamepita. Binadamu tuna uhakika wa maisha ya leo, yajayo hatuyajui.

Juzi kupitia baadhi ya magazeti niliona habari juu ya wewe kutamani mtoto. Kimsingi nilipenda na kuona kwamba una nia ya dhati kumpata. Pamoja na nia yako hiyo nzuri, nilipata shaka kidogo kama kauli yako hiyo ulikuwa unamaanisha au ulitamka tu ili mradi kwani kumbukumbu inaonesha uliwahi kupata ujauzito na kwa sababu ambazo hazieleweki, mimba zikayeyuka.

Kudhihirisha hilo nilisemalo, ninakumbuka maneno ya aliyekuwa mpenzi wako, Nasibu Abdul ‘Diamond’ aliyoyazungumza hivi karibuni kupitia Global TV Online.
Alifunguka mengi kuonesha hisia zake juu ya suala la kutamani kupata mtoto lakini kimsingi, aliumia kwa kile alichosema kwamba ulimfanyia ujanjaujanja na akajikuta amepoteza kiumbe ambacho alikuwa na imani kwamba utamzalia.

Mbaya zaidi alidai si mara moja, alisema kutokana na sababu za nyinyi mabinti wa mjini kupenda kula ujana, wengi wenu huwa hampendi kuzaa na ndiyo maana hata ilipotokea amekupa mimba ya pili, nayo ukaitoa pasipo kuwa na sababu za msingi.

Kuonesha msisitizo wa namna ambavyo Diamond aliumia, ngoja nimnukuu hapa:
“Nikampa mimba ya kwanza, sikuamini ikabidi twende naye hadi hospitali, tukapima akaambiwa anayo...nikafurahi nikampiga na ndinga mpya siku hiyohiyo. Nikamwambia mama tulia unizalie mwanangu.

“Sikukaa sana akaniletea maneno oooh mara hivi mara vile, eti imetoka. Nikasema poa, labda haikuwa riziki. Nikampa ya pili nayo pia akatoa. Nikasema bora niachane naye. Na huo ndiyo ukawa mwisho wa mimi na Penny.”

Kwa maneno hayo ya Diamond inaonesha ni dhahiri ulimfanyia ujanjaujanja ukatoa mimba zake kitu ambacho kinaweza kukusumbua sana akilini mwako. Kutoa mimba si jambo jema hata kidogo, ikifanyika vibaya inaweza kukusababishia matatizo kiafya.

Kwa nini lakini uliamua kumfanyia kitu kama hicho? Kwa kuwa yaliyopita si ndwele, tugange yajayo. Nikushauri tu, kwa kuwa kwa sasa unahitaji mtoto basi tusije tukasikia hadithi kama hizo tulizosikia. Zaa bwana, wenzio wanawatafuta watoto miaka na miaka hawawapati.

Kama haupo tayari kuzaa basi usikubali kupata ujauzito, mimba ni kitu ambacho kinazuilika. Ni vyema ukajizuia hadi muda ambao kweli utakuwa tayari.