Thursday, February 5, 2015

MWENYEKITI CUF ALIZIMIA MAHAKAMANI!

Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Kata ya Sandare, Temeke jijini Dar, Abina Ally akiwa Mahakamani.
Denis Mtima/Amani
MAJANGA! Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Kata ya Sandare, Temeke jijini Dar, Abina Ally Abina amejikuta akipandwa na presha kisha kuzimia katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Tukio hilo ambalo lilikuwa gumzo lilijiri hivi karibuni mahakamani hapo ambapo Abina alikuwa miongoni mwa wafuasi 30 waliokamatwa kwa madai ya kufanya maandamano kutoka Temeke kwenda Zakhem na Mwenyekiti wa CUF Taifa, Prof. Ibrahim Haruna Lipumba.
MKASA MZIMA
Akisimulia mkasa mzima, mmoja wa wafuasi hao ambaye hakutaja jina alisema kuwa, tukio hilo la mwenyekiti wao kupatwa na presha na kuzimia lilitokana na kutomwamini mdhamini wake, Maulid Ngoyogo katika kutoa maelezo baada ya kuitwa na hakimu ili apatiwe dhamana.
Mwenyekiti huyo, Abina Ally akiamshwa kwa kumwagiwa maji.
HOFU YA KURUDISHWA RUMANDE
Katika msala huo, kila mtuhumiwa alipendekeza mdhamini wake ambapo walikuwa wakiitwa kwa zamu.
“Hali hii imetokana na kuhofia mdhamini wake kushindwa kujieleza kiufasaha huku akihofia kurudishwa rumande tena kwa kushindwa kutoa maelezo sahihi,” alisema mfuasi huyo.
AMWAGIWA MAJI, AZINDUKA
Hadi gazeti hili linaondoka kwenye viunga vya mahakama hiyo, jamaa huyo alimwagiwa maji na kuzinduka ambapo aliendelea na taratibu za dhamana huku akisubiri kesi hiyo ya maandamano bila kibali kuendelea kuunguruma.
Hata hivyo, hakuwa tayari kuzungumza na mwanahabari wetu juu ya tukio hilo.