Friday, March 27, 2015

SAKATA LA ESCROW: AFISA MTENDAJI MKUU WA RITA AFIKISHWA MAHAKAMANI


Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU, leo imemfikisha katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Afisa Mtendaji Mkuu wa wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini-RITA, Bw. Philip Saliboko kwa tuhuma za kupokea rushwa.

Kwa mujibu wa mwendesha mashtaka waTAKUKURU Bw. Denis Lekayo, Saliboko anatuhumiwa kupokea rushwa ya shilingi milioni arobaini, laki nne na elfu ishirini na tano kutoka kwa mfanyabiashara Bw. James Burchard Rugemalila.
 
Kwa mujibu wa Lekayo, fedha hizo ni sehemu ya zilizokuwa fedha za Escrow na kwamba afisa mtendaji huyo wa Rita alipokea fedha hizo kupitia akaunti yake iliyokuwa katika benki ya Mkombozi.
 
Aidha, mahakama kupitia kwa hakimu mkazi Thomas Simba, imemwachia kwa dhamana Bw. Saliboko baada ya kutimiza masharti ya dhamana ambayo ni pamoja na kuwa na wadhamini wawili ambao kila mmoja alitakiwa awe na fedha taslim shilingi milioni 22.