Wednesday, June 17, 2015

SHEHE AMUONYA SHILOLE BAADA YA KUTANGAZAA KUWA ANASWALI SWALA TANO

Mayasa Mariwata
Shehe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Mussa Salim, amemjia juu staa wa sinema na Bongo Fleva, Zuwena Mohammed a.k.a Shilole au Shishi Baby baada ya kutangaza kuwa anasali swala tano, kauli ambayo inalenga kudhalilisha Uislam kutokana na skendo zake hasa kukaa mtupu, jambo ambalo ni kukiuka maadili ya binti wa Kiislam.
Staa wa sinema na Bongo Fleva, Zuwena Mohammed a.k.a Shilole au Shishi Baby.
Hivi karibuni, huku akiwa na skendo ya kutia aibu Ulaya, Shilole alidai yeye ni Muislam safi na kwamba ni swala tano, jambo lililoibua mjadala mzito kwa mashabiki wake kwa kuwa alichokisema hakiendani na muonekano wake.
Akizungumza na gazeti hili baada ya kuibuka kwa ishu hiyo, shehe huyo aliamua kuingilia akieleza kwamba sifa za Muislam anayesali swala tano haziendani kabisa na yeye na anapaswa kujitazama upya.
“Kwa kuwa yeye mwenyewe ndiye kasema, hatuwezi kumbishia, isipokuwa kwa jinsi alivyo ukianzia suala la mavazi ni wazi anaidhalilisha dini ya Kiislam kwa sababu Muislam ambaye ni mcha Mungu kwa kiasi hicho, anatakiwa ajisitiri kimavazi.
Shehe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Mussa Salim.
“Kama haitoshi ukitazama hata matendo yake mfano ile shoo aliyoenda kufanya kule Ubelgiji (Ulaya) na kuonekana sehemu ya matiti haikustahiki kabisa kwani ameenda kinyume na matakwa ya dini yake, inawezekana tukawa tunamlaumu lakini huenda akawa hana mafunzo ya kutosha ya kidini na kujua anapaswa awe vipi ili kuendana na sheria za Dini ya Kiislamu hususan kwa mtu ambaye ameamua kujitakasa na maovu na kumsujudia Mungu,” alisema shehe huyo anayeheshimika.
Alisema hapendi ‘kumjaji’ mtu aliyeamua kubadilika kwa kuacha mambo ya dunia na kumfuata Mungu, hivyo alimpa mwaliko maalum Jumapili afike kwenye Viwanja vya Karimjee jijini Dar ambako kulikuwa na mafunzo maalum yaliyotolewa kwa Waislam wote kwa ajili ya kujiandaa na Mwezi Mtukufu wa Ramadhani (haikujulikana kama Shilole alikwenda).