Thursday, June 2, 2016

Mbowe: Tupo Tayari Kutimuliwa Wote Bungeni Sababu ya Naibu Spika Tulia Ackson

Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson sasa amesababisha makubwa zaidi; wabunge kutoka vyama vya upinzani wako radhi kutimuliwa wote iwapo kiongozi huyo ataongoza vikao vyote vilivyosalia na wao kuendelea na msimamo wao wa kumsusia.


Jana, Dk Ackson aliingia kuongoza kipindi cha maswali na majibu na wabunge wote wa vyama vya upinzani wakatoka ndani ya ukumbi na alipomuachia mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge kuendelea na shughuli zilizosalia, walirejea ukumbini.


“Kama Naibu Spika atakuwepo kwenye kile kiti, hatatuona bungeni, hata kama ni leo, ni kesho hata Bunge lote. Tuko tayari kuchukua gharama hiyo,” alisema kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe akiwa nje ya ukumbi wa Bunge baada ya kuongoza wabunge wenzake kutoka ukumbini wakati wa kipindi cha maswali na majibu.


Kauli hiyo ya Mbowe imekuja siku moja baada ya Dk Ackson kukataa Bunge kujadili sakata la wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) waliotimuliwa kwa maelezo kuwa hawafundishwi kwa muda mrefu kutokana na walimu wao kugoma wakidai malimbikizo yao.


Kitendo cha Dk Ackson kukataa hoja hiyo ijadiliwe, kilisababisha vurugu bungeni kiasi cha kuita askari kuingia kuwatoa wabunge waliokuwa wakipiga kelele na baadaye kuwaamuru waliokataa kukaa waondoke ukumbini.


Wakiwa nje, walifikia uamuzi wa kususia vikao vyote vitakavyoongozwa na Naibu Spika na wakaanza kutekeleza uamuzi huo jana asubuhi.


Kauli ya Mbowe pia imekuja siku moja baada ya Kamati ya Maadili, Kinga na Haki za Bunge kuwasimamisha wabunge saba kutoka vyama vya upinzani kuhudhuria vikao vya kuanzia mkutano huu hadi ujao kwa maelezo kuwa walifanya fujo wakati wakipinga hoja ya Serikali ya kusimamisha matangazo ya moja kwa moja ya baadhi ya shughuli za Bunge.


Jana, Mbowe alisema wako tayari kutimuliwa wote kama uamuzi huo utawapendeza viongozi wa Bunge kwa kuwa siasa inaweza kufanywa ndani na nje ya Bunge.


Mbowe alisema kuwa hali ilishafika hatua nzuri ya kujenga demokrasia nchini na kwamba pamoja na matatizo yaliyokuwepo, hali ilikuwa ikienda vizuri.


“Lakini tangu kuingia kwa Serikali ya Awamu ya Tano mnaweza kuona Bunge limegeuka kituko. Bunge limegeuka mahali pa kukomoana. Bunge limekuwa mahali pa kutishana,” alisema Mbowe.

“Naibu Spika anaamua kusitisha mjadala wa maana ili apate muda wa kuwadhibiti na kuwafukuza wabunge bungeni na anaona sifa. 


Tunaacha kujadili hoja ya msingi kama mambo ya Udom. Watoto wadogo wanalala nje haoni ni muhimu, anaona muhimu ni kuwafukuza wabunge wa upinzani.” 

Mbowe, ambaye pia ni mbunge wa Hai, alisema hawezi kukaa, kumsikiliza na kumheshimu Dk Ackson, bali wapinzani wataheshimu anayewaheshimu bila kujali anatoka chama gani na hawatamuheshimu asiyewaheshimu bila kujali cheo chake.


“Sasa leo (jana) tumekataa kushiriki kipindi cha maswali na majibu kwa sababu yeye (Dk Ackson) anasimamia kipindi hicho na akitoka tutarudi bungeni. 


Akija mwenyekiti, akija Spika mwenyewe tutarudi bungeni. Lakini kama Naibu Spika atakuwepo kwenye kile kiti hatatuona bungeni, hata kama ni leo, ni kesho hata Bunge lote. Tuko tayari kuchukua gharama hiyo,” alisema Mbowe.