IMEVUJA! Siku chache baada ya kifo cha mwongozaji na mwigizaji wa filamu Bongo, Adam Philip Kuambiana, daktari mkubwa wa mastaa ameibuka na kudai marehemu alijiua mwenyewe.
Kwa mujibu wa daktari huyo ambaye hakupenda jina lake lichorwe gazetini kutokana na maadili ya taaluma yao kuficha siri ya mgonjwa, siku moja kabla ya kifo (Ijumaa ya Mei 16, mwaka huu), marehemu alimpigia simu na kumwambia amekunywa dawa za malaria aina ya Fansidar lakini pia amekunywa pombe.
ILIVYOKUWA
Daktari huyo alieleza kuwa, marehemu alimpigia simu kumuomba ushauri juu ya nini cha kufanya na kama kuna madhara yoyote juu ya pombe hizo na dawa alizokunywa.
AMSHAURI KWENDA HOSPITALI
Akizidi kuzungumzia tukio hilo, daktari alikwenda mbele kwa kusema licha ya msanii huyo kuwa na ‘masikhala’ mara kwa mara, lakini kwa kuwa alimwambia jambo ambalo linahusu uhai wake, alimshauri kwenda hospitali iliyo karibu ili akaonane na daktari kwa ajili ya kuangalia uwezekano wa kutoa sumu kwani kitaalam mtu anapokunywa pombe akiwa amemeza dawa za aina hiyo vyote hugeuka kuwa sumu.
MAZINGIRA YA KIFO
Kwa mujibu wa mtu ambaye alikuwa karibu na Kuambiana siku ya tukio ambaye naye hakutaka kutajwa jina gazetini, marehemu asingekufa ghafla kama tatizo alilokuwa nalo lingekuwa la vidonda vya tumbo ambavyo vilikuwa vikimsumbua kwa muda mrefu.
DAKTARI AWAASA MASTAA
Katika hatua nyingine, daktari huyo aliwashauri mastaa wengine kuwa makini kwani mara kadhaa amepata kesi za namna hiyo ambapo wanakunywa pombe vilabuni usiku huku wakiwa katika dozi ya ugonjwa fulani.
DAKTARI MUHIMBILI ANENA
Ili kuzidi kupata undani wa mazingira ya kifo cha Kuambiana, Amani lilimtafuta daktari mwingine mtaalam wa magonjwa ya binadamu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH). Naye kwa sharti la kutotaja jina alieleza madhara ya mtu kunywa pombe akiwa kwenye dozi.
JB AANGUKA GHAFLA, AZUA HOFU
Wakati shughuli za kuaga mwili zikiendelea juzi, Jumanne katika Viwanja vya Leaders, Kinondoni jijini Dar, nguli wa filamu nchini ambaye alikatisha ziara yake ya kikazi nchini Uturuki kwa ajili ya kuja kumzika Kuambiana, Jacob Steven ‘JB’, alipewa kipaza sauti ili amzungumzie marehemu ambapo akiwa katikati ya kuongea alianguka ghafla.
Umati wa watu uliokusanyika viwanjani hapo uliingia hofu na kushindwa kuelewa amepatwa na nini lakini haikuchukua muda mrefu akasaidiwa na watu na kuendelea na shughuli nyingine.
MASTAA WAONGOZA KWA VILIO
Mastaa mbalimbali wa Bongo Movies wakiongozwa na Wema Sepetu ‘Beautiful Onyinye’, Aunt Ezekiel, Blandina Chagula ‘Johari’, Miriam Jolwa ‘Jini Kabula’ waliongoza kwa kulia viwanjani hapo hadi walipofika makaburini, Kinondoni.
Mbali na mastaa hao kuangusha vilio, Mkurugenzi wa Aset, Asha Baraka alijikuta akishindwa kuaga kwa kuhofia kuuona mwili wa marehemu na kudai huwa akitazama maiti anamuota kwa zaidi ya mwezi mmoja.
Marehemu Kuambiana ambaye alikuwa nguzo muhimu katika ‘ku-dairekti’ filamu, alipatwa na mauti katika Gesti ya Silvarado, Sinza- Kwaremmy jijini Dar. Mungu ailaze pema peponi roho ya marehemu. Amina.