Thursday, May 22, 2014

Daktari: ADAM KUAMBIANA Alijiua….Alikunywa Fansida na kusindikiza na Pombe..!

IMEVUJA! Siku chache baada ya kifo cha mwongozaji na mwigizaji wa filamu Bongo, Adam Philip Kuambiana, daktari mkubwa wa mastaa ameibuka na kudai marehemu alijiua mwenyewe.
Kwa mujibu wa daktari huyo ambaye hakupenda jina lake lichorwe gazetini kutokana na maadili ya taaluma yao kuficha siri ya mgonjwa, siku moja kabla ya kifo (Ijumaa ya Mei 16, mwaka huu), marehemu alimpigia simu na kumwambia amekunywa dawa za malaria aina ya Fansidar lakini pia amekunywa pombe.
kuambiana
Marehemu Adam Kuambiana enzi za uhai wake.

ILIVYOKUWA

Daktari huyo alieleza kuwa, marehemu alimpigia simu kumuomba ushauri juu ya nini cha kufanya na kama kuna madhara yoyote juu ya pombe hizo na dawa alizokunywa.
“Aliniuliza kama kuna madhara yoyote ambayo anaweza kuyapata kwa kuwa alikuwa amekunywa fansidar kwa ajili ya malaria kisha akapata kiu ya bia na kuamua kunywa,”alisema daktari huyo.

AMSHAURI KWENDA HOSPITALI

Akizidi kuzungumzia tukio hilo, daktari alikwenda mbele kwa kusema licha ya msanii huyo kuwa na ‘masikhala’ mara kwa mara, lakini kwa kuwa alimwambia jambo ambalo linahusu uhai wake, alimshauri kwenda hospitali iliyo karibu ili akaonane na daktari kwa ajili ya kuangalia uwezekano wa kutoa sumu kwani kitaalam mtu anapokunywa pombe akiwa amemeza dawa za aina hiyo vyote hugeuka kuwa sumu.

Alisema kutokana na jinsi alivyozidi kumsimulia hali aliyonayo, aliamini kwamba marehemu alikuwa anamaanisha alichokuwa akikisema hivyo ikabidi amsisitize kuwahi hospitali haraka.
“Nilimwambia awahi hospitalini haraka kwani nilijua fansidar ni kali na si dawa ya kufanyia mchezo. Lakini kesho yake nilipopata taarifa za kifo chake niliumia sana japokuwa nilijua amejiua kwa kuchangaya fansidar na bia maana mchanganyiko wa sumu yake mwilini ni mkali sana,” alisema daktari huyo huku akisisitiza kusitiriwa kwa jina lake.

MAZINGIRA YA KIFO

Kwa mujibu wa mtu ambaye alikuwa karibu na Kuambiana siku ya tukio ambaye naye hakutaka kutajwa jina gazetini, marehemu asingekufa ghafla kama tatizo alilokuwa nalo lingekuwa la vidonda vya tumbo ambavyo vilikuwa vikimsumbua kwa muda mrefu.
“Siku ile marehemu alikuwa na pesa, alikunywa sana pombe kutoka asubuhi mpaka usiku mwingi, alikuwa anakula kila anapojisikia sasa hatuelewi ni kitu gani kilitokea maana haiwezekani mtu akutwe anaendesha na kutapika damu pasipo kuwa na sumu mwilini,”alisema mtu huyo.

DAKTARI AWAASA MASTAA

Katika hatua nyingine, daktari huyo aliwashauri mastaa wengine kuwa makini kwani mara kadhaa amepata kesi za namna hiyo ambapo wanakunywa pombe vilabuni usiku huku wakiwa katika dozi ya ugonjwa fulani.

“Mimi nawaambia ndugu zangu, hasa mastaa waache tabia ya kunywa pombe wakiwa katika dozi, starehe zipo tu. Ni vyema wakawa wanauliza kwa wataalam wa afya pindi wanapokuwa wamemeza dawa za aina yoyote, nguvu ya dawa inatofautiana kulingana na ugonjwa husika na muda wa kukaa mwilini,” alisema daktari huyo.

DAKTARI MUHIMBILI ANENA

Ili kuzidi kupata undani wa mazingira ya kifo cha Kuambiana, Amani lilimtafuta daktari mwingine mtaalam wa magonjwa ya binadamu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH). Naye kwa sharti la kutotaja jina alieleza madhara ya mtu kunywa pombe akiwa kwenye dozi.

“Unapokunywa dawa hususan hiyo fansidar, inakaa katika mwili kwa takriban siku saba hivyo mgonjwa anapokunywa pombe ndani ya siku hizo, pombe inapochanganyika na dawa katika mzunguko wa damu hugeuka kuwa sumu na mgonjwa ana uwezekano wa kupoteza maisha endapo asipowahishwa hospitalini,” alisema daktari huyo na kuongeza:
“Wengi huwa wanajisahau na kunywa pombe kabla ya siku saba lakini wengine huwa wanakunywa pombe makusudi pale tu wanapoanza kupata ahueni ya ugonjwa pasipo kutambua nguvu ya dawa bado ipo mwilini mwake na madhara yake ndiyo hayo.”

JB AANGUKA GHAFLA, AZUA HOFU

Wakati shughuli za kuaga mwili zikiendelea juzi, Jumanne katika Viwanja vya Leaders, Kinondoni jijini Dar, nguli wa filamu nchini ambaye alikatisha ziara yake ya kikazi nchini Uturuki kwa ajili ya kuja kumzika Kuambiana, Jacob Steven ‘JB’, alipewa kipaza sauti ili amzungumzie marehemu ambapo akiwa katikati ya kuongea alianguka ghafla.
Baadhi ya mabaunsa na wasanii wenzake wakimnyanyua JB,baada ya kuzidiwa na kudondoka chini.
Baadhi ya mabaunsa na wasanii wenzake wakimnyanyua JB,baada ya kuzidiwa na kudondoka chini.

Umati wa watu uliokusanyika viwanjani hapo uliingia hofu na kushindwa kuelewa amepatwa na nini lakini haikuchukua muda mrefu akasaidiwa na watu na kuendelea na shughuli nyingine.

MASTAA WAONGOZA KWA VILIO

Mastaa mbalimbali wa Bongo Movies wakiongozwa na Wema Sepetu ‘Beautiful Onyinye’, Aunt Ezekiel, Blandina Chagula ‘Johari’, Miriam Jolwa ‘Jini Kabula’ waliongoza kwa kulia viwanjani hapo hadi walipofika makaburini, Kinondoni.
Mbali na mastaa hao kuangusha vilio, Mkurugenzi wa Aset, Asha Baraka alijikuta akishindwa kuaga kwa kuhofia kuuona mwili wa marehemu na kudai huwa akitazama maiti anamuota kwa zaidi ya mwezi mmoja.
Marehemu Kuambiana ambaye alikuwa nguzo muhimu katika ‘ku-dairekti’ filamu, alipatwa na mauti katika Gesti ya Silvarado, Sinza- Kwaremmy jijini Dar. Mungu ailaze pema peponi roho ya marehemu. Amina.