Wednesday, October 22, 2014

HEEE! MUME AMSHTAKI MKEWE KWA WIZI WA MTOTO WAO

KIOJA! Jalada la kesi namba MAG/RB/8329/2014- WIZI kwenye Kituo cha Polisi cha Magomeni, Dar, limefunguliwa na mwanaume aitwaye Rashidi akimshitaki mkewe, Fatuma Ally akimtuhumu kwa wizi wa mwanaye Zainabu Rashidi aliyemwandikisha jina la mwanaume mwingine aliyetajwa kwa jina la Paulo Mlela.
Bw. Rashidi anayemshitaki mkewe, Fatuma Ally kwa wizi wa mwanaye Zainabu Rashidi.
Kwa mujibu wa Rashidi anayeishi na familia yake maeneo ya Tandale-Yemen, Dar, sakata hilo lilijiri wiki mbili zilizopita baada ya yeye kwenda katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya kumchukulia mwanaye cheti cha kuzaliwa.
Rashidi alisema kwamba alipofika Muhimbili alishangaa alipojikuta akiwekwa chini ya ulinzi na kuhojiwa kwa muda na madaktari akidaiwa ni mwizi wa mtoto.Alisema, aliwaonyesha kadi ya kliniki ya mtoto Zainabu yenye jina lake (Rashidi) akiwa ndiye baba mzazi wa mtoto huyo, jambo ambalo madaktari hao walilishangaa.Bw. Rashidi akiwa amembeba mwanaye, Zainabu Rashidi.
Hata hivyo, madaktari hao walimwachia kwa sharti la kutopatiwa cheti cha kuzaliwa hadi ampeleke Paulo Mlela ambaye jina lake lipo kwenye makabrasha hospitalini hapo likionyesha naye ni baba mzazi wa Zainabu.
Katika kudadisi, Rashidi alionyeshwa fomu ya discharge (kuruhusiwa) baada ya mkewe kujifungua iliyoonyesha jina la Paulo Mlela kama mume wa Fatuma badala ya jina lake, jambo lililomchanganya na kuamua kufuatilia ukweli kwa mkewe ambaye alikataa tuhuma hizo na kudai kuwa hakuwa akijielewa wakati fomu hiyo ilipokuwa inajazwa kwa kuwa alikuwa ametoka kujifungua.
Cheti cha kliniki kinachoonyesha wazazi halisi wa Mtoto Zainabu Rashidi.
Rashidi alisema kuwa siku mkewe alipokuwa anajifungua yeye na ndugu zake wa karibu walikuwa safarini mazishini hivyo huenda mwanaume huyo alipata nafasi ya kuingiza jina lake. Rashidi alisema aliamua kumtafuta Paulo kisirisiri ndipo akagundua kuwa anaishi mtaa wa pili kutoka nyumbani kwake na mara kadhaa aliwahi kumwona akiwa na mkewe.
Fomu ya discharge (kuruhusiwa) baada ya mkewe kujifungua ikionyesha jina la Paulo Mlela kama mume wa Fatuma badala ya jina la bw. Rashid.
“Jamaa nilikuwa simfahamu kumbe anaishi mtaa wa pili kutoka nyumbani kwangu. Mara kadhaa nilishawahi kumwona na mke wangu lakini sikujua kama kuna jambo linaendelea.“Hadi sasa najiuliza ilikuwaje mpaka mke wangu amwandike yeye kama baba mzazi wa mtoto wangu wakati mwenyewe nipo?” Alihoji Rashidi bila kupata jibu.
Akizungumzia hatua ambazo alizichukuwa, Rashidi alidai kuwa amelifikisha suala hilo polisi na baraza la kata ambako linashughulikiwa kupitia ustawi wa jamii.Rashidi aliongeza kwamba, kwa sasa mkewe ameondoka nyumbani.
Mke wa Bw. Rashidi anayetuhumiwa kwa wizi wa mtoto.
Nao ndugu wa mwanamke walipotafutwa kulizungumzia suala hilo, walisema wanamtambua Rashidi kama baba halali wa mtoto Zainabu huku wakimkataa Paulo. Waliomba kwamba, kwa kuwa Rashidi amejua ukweli na kwamba mtoto ni wake basi akae na mkewe wayamalize maisha yaendelee kwani wametoka mbali.