Friday, October 24, 2014

MKE ASIMULIA MATESO ALIYOPATA YP

MKE wa aliyekuwa memba wa Kundi la TMK Family, Yessaya Ambikile ‘YP’ aliyefariki katika Hospitali ya Temeke, jijini Dar, Sakina Robert amefungukia mateso aliyopitia mumewe hadi umauti ulipomkuta usiku wa Oktoba 20, mwaka huu.
Mke wa marehemu Yessaya Ambikile ‘YP’ aliyefariki katika Hospitali ya Temeke, jijini Dar, Sakina Robert akilia kwa uchungu katika msiba uliotokea.
Akizungumza na waandishi wetu nyumbani alipokuwa akiishi na marehemu, Keko jijini Dar, Sakina alisema mumewe ameteseka kwa muda mrefu akisumbuliwa na ugonjwa wa kifua kikuu ambapo alitibiwa na kumaliza dozi kabla ya kuugua ugonjwa wa Pneumonia ambao ndiyo uliomsababishia kifo chake.
Wasanii na marafiki wa marehemu Yessaya Ambikile ‘YP’ wakitoa heshima zao za mwisho kwake.
Sakina alisema, awali YP alikuwa akilalamika kubanwa na kifua kiasi cha kupumua kwa tabu hivyo akashirikiana na familia ya mumewe kumkimbiza hospitali kwa ajili ya matibabu.
Waombolezaji wakihuzunika kumpoteza marehemu Yessaya Ambikile ‘YP’.
“Mwezi wa tatu mwaka huu, YP aligundulika na ugonjwa wa kifua kikuu na tayari alianza matibabu, alimaliza dozi mwezi wa tisa na hali yake ghafla ikabadilika na kuanza kubanwa na kifua. Tulimpeleka Hospitali ya Temeke, Oktoba 19 mwaka huu na akaonekana ana Pneumonia, Oktoba 20 usiku ndipo akafariki,” alisema mke wa marehemu kwa uchungu.
Mkali wa Bongo Fleva na Swahiba wa Karibu wa Yessaya Ambikile ‘YP’, Chege akitoa yake machache katika msiba huo.
Meneja wa Kruu ya TMK Family, Said Fella aliyeambatana na rafiki wa karibu wa marehemu Said Chigunda ‘Chegge’ alimuelezea YP kama shujaa, aliyekuwa tayari kupambana muda wote na kuongeza kuwa YP alifariki wakati akiwa bado hajamaliza kurekodi ngoma yao iliyopewa jina la Wazee wa Jiji waliyofanya na Kundi la Tip Top Connection.
Waombolezaji wakiuweka mwili wa marehemu Yessaya Ambikile ‘YP’ akburini.
Enzi za uhai wake, marehemu YP amesikika katika ngoma kali ikiwemo, Dar Mpaka Moro, Umewaona, Twenzetu Kichwa Kinauma, Umri, Pumzika na Tunafurahi.
YP alizikwa juzi katika Makaburi ya Chang’ombe jijini Dar, Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina.