Wednesday, October 8, 2014

TANZANIA YANG’ARA UZINDUZI WA BIG BROTHER AFRICA, MTANZANIA ACHAGULIWA KUWA HEAD OF HOUSE

Shindano linalopendwa  na wengi  barani Afrika, maarufu la Big Brother Afrika ambalo kwa mwaka huu ni la msimu wa 9 likijulikana kama Big Brother Hotshot lililoanza usiku wa kuamkia leo Tanzania imeng’ara hasa kwa washiriki wake kufanya vizuri katika muonekano wa awali sambamba na shoo iliyopigwa na mwanamuziki Nasseb Abdul ‘Diamond’ aliyeteka umati uliohudhuria uzinduzi huo.

Halfa hiyo ya masaa mawili ambayo imeweza kushuhudia washiriki  26,  imekuwa  gumzo pale washiriki wanaoiwakilisha Tanzania msimu huu wa 9, Laveda na Idriss wakifanya kweli katika utambulisho wao huku mwanamuziki Diamond akikonga vilivyo na wimbo wake wa ‘My Number One’.

Tanzania imekuwa na bahati ya kipekee kwa mshiriki wake huyo, Laveda ambapo aliteka umati mkubwa kwa kuonesha uhodari wake wa kupuliza “Saxophone”, hali iliyopelekea kupigiwa kura nyingi huku akishangiliwa kwa shangwe muda wote.
Kura hizo alizopigiwa Laveda na kuwa juu ya washiriki wote 26, pia zimemfanya awe Mkuu wa jumba hilo ‘Head of the House’ mpaka hapo itakapoamuliwa na Biggy. Kura alizopigiwa Laveda ni 85.0 huku mshiriki wa Kenya, Sabina akipata kura 78.3, ambaye yeye alionyesha uwezo wake wa kuchekesha kwa kutumia maneno.