Sunday, December 21, 2014

RAIS KIKWETE KULIHUTUBIA TAIFA TAREHE 22, JUMATATU MCHANA


Rais Kikwete ameahirisha kulihutubia taifa   kupitia "Wazee wa Dar" ambapo sasa ataongea nao Jumatatu wiki ijayo(Disemba 22, 2014). Ikulu imethibitisha na kusema muda utatangazwa.
 
Rais kikwete jana tarehe 19 alitarajiwa kulihutubia taifa kupitia wazee wa mkoa wa Dar es salaam katika mkutano wake ambao ulikuwa ufanyike katika ukumbi wa  Hotel ya Blue Pearl,Ubungo jijini Dar es salaam.
 
Katika mkutano wake huo Rais Kikwete alitazamia kuzungumzia  mustakabali wa nchi sambamba na kuweka wazi juu ya sakata la utekelezaji wa maazimio nane likiwamo la Bunge la kuwawajibisha viongozi waliotajwa katika sakata la uchotwaji wa fedha bilioni 360 katika akaunti ya Tegeta Escrow Pamoja na mambo mengine.
 
Katika maazimio nane ya bunge yaliyopendekezwa yalitaka viongozi waliotajwa katika ripoti hiyo kwa tuhuma za uchotwaji wa fedha kuchukuliwa hatua za kinidhamu na hata wanapo bainika kufilisiwa mali zao na kushitakiwa katika vyombo husika kwa kuonekana kulihujumu taifa katika sakata hilo la uchotwaji wa fedha akaunti ya Escrow.
 
Rais pia alipanga kuzungumzia juu ya Sekta ya Elimu pamoja na agizo lake la ujenzi wa maabara kwa shule za sekondari nchini,Upigaji kura za maoni kuhusu katiba Mpya utakao fanyika Aprili 30 pamoja na daftari la wapiga kura.
 
Hata hivyo Katika Hotuba hiyo Rais aliazimia kuelezea uchaguzi wa serikali za Mitaa ulivyo fanyika ambao ulionekana kukumbwa na dosari kadhaa katika  vituo vya kupigia kura katika sehemu mbali mbali za nchi ulipo kuwa ukifanyika uchaguzi huo ambao uliweza kugharimu maisha ya watu .