Vyama vya siasa vinavyounda UKAWA vitatumia nguvu ya umma kuing'oa madarakani serikali ya chama cha mapinduzi kwa kuwapigia kura ya kutokuwa na imani waziri mkuu na Rais Kikwete kama leo haitatekeleza maazimio ya bunge ya kuwawajibisha wote waliohusika na sakata la uchotwaji wa fedha akaunti ya Tegeta Ewscrow.
Naibu katibu mkuu wa chadema Mh. John Mnyika amesema hayo katika mkutano wa hadhara katika manispaa ya moshi kuwapongeza wananchi wa manispaa hiyo kwa kuonyesha imani na chama hicho na kukipatia ushindi wa mitaa 31 dhidi ya 29 ya CCM katika uchaguzi wa serikali za mitaa.
Mh. Mnyika amesema, kura hizo zitapigwa na wabunge wa ukawa ambao pia watafanya kazi ya kuwahamasisha wananchi wajiandikishe kwa wingi katika daftari la wapiga kura ili kuipigia kura ya hapana katiba inayopendekezwa mwezi aprili mwaka 2015 na kuwawezesha pia kupiga katika uchaguzi mkuu ujao na kuing'oa CCM.
Mwenyekiti wa chadema mkoani kilimanjaro Mh.Philemon Ndesamburo amewataka wananchi wakubali kufanyika mabadiliko katika uchaguzi mkuu ujao ili UKAWA ambayo imedhamiria kuchukua madaraka ya nchi iweze kuwaletea maendeleo ya kweli.