Thursday, May 21, 2015

NIGERIA; KISIMA CHA MATAJIRI AFRIKA

Mfanyabiashara Mnigeria, Aliko Dangote.
Nyemo chilongani
Unapoizungumzia Nigeria mbele za watu, wengine wanajua kwamba unaizungumzia moja ya nchi iliyojaza matapeli wengi wa mitandaoni huku wengine wakijua unaizungumzia nchi iliyokuwa na wasomi wengi barani Afrika, ila kwa wengine, watajua kwamba unaizungumzia nchi yenye matajiri wengi katika bara hili.
‘P Square’.
Nchi hii iliyopo Afrika Magharibi ndiyo nchi yenye matajiri wengi barani Afrika, kuanzia viongozi wa siasa akiwemo rais aliyepita, Jonathan, wafanyabaishara, wanamuziki na watu wengine. Ni nchi pana, yenye watu wengi huku tatizo la ajira likiwa kubwa kiasi kwamba unaweza kumkuta mtu mwenye digrii lakini anashona viatu barabarani.
Hebu tushuke hapa chini kuona matajiri wengi wa nchi hiyo ngazi mbalimbali.
WAFANYABIASHARA
Unapozungumzia matajiri wakubwa barani Afrika, moja kwa moja utamtaja tajiri namba moja Afrika na wa 67 duniani, Mnigeria, Aliko Dangote.  Katika wafanyabiashara kumi wenye fedha nyingi barani Afrika, Nigeria imetoa wawili akiwemo huyo Dangote mwenye utajiri wa dola bilioni 21 (zaidi ya shilingi trilioni 45) na Mnigeria mwingine aitwaye Mike Adenuga mwenye utajiri wa dola bilioni 4 (zaidi ya shilingi trilioni 9)
WANAMUZIKI
Nigeria haikuishia hapo tu, pia ina wanamuziki wenye fedha nyingi kuliko wote Afrika. Japokuwa namba moja inashikwa na Msenegal, Youssou N’Dour, lakini kuna wanamuziki wanne kati ya kumi Afrika wanaotoka nchini Nigeria ambao ni Peter na Paul Okoye ‘P Square’ (2) ambao wamesimama kama kundi na wanamiliki nyumba yao kubwa ya kifahari na ndege binafsi,  Innocent Ujah Idibia ‘2 Face Idibia’,  Olubankole Wellington ‘Banky W’ (8) na Oladapo Daniel Oyebanjo ‘D’banj’ ambao wote hao wanamiliki nyumba za kifahari, magari ya bei mbaya na wana mashabiki wengi pia katika kazi zao.
Mchungaji T.B Joshua.
WACHUNGAJI
Ili kuonyesha kwamba nchi hiyo ni nchi yenye matajiri wengi, hata wachungaji nao hawapo mbali, katika orodha ya wachungaji kumi wenye mkwanja mkubwa duniani, Nigeria inatoa wachungaji watano wanaokimbiza huku namba moja ikishikiliwa na mchungaji David Oyedebo wa kanisa la Faith World Outreach Ministry ambaye ana utajiri wa dola milioni 150 (zaidi ya shilingi bilioni 300).
Wachungaji wengine wenye mkwanja wa maana kutoka Nigeria ambao wapo kwenye orodha hiyo ni Chris Oyakhilom kutoka katika Kanisa la Christ Embass anashika namba 2 duniani ambaye ana utajiri wa dola 120 (zaidi ya shilingi bilioni 250) . 
T.B Joshua  wa kanisa la The Synagogue, Church of All Nations  na anashika namba 7 duniani huku akiwa na utajiri wa dola milioni 100 (zaidi ya shilingi bilioni 200). Nchungaji Matthew Ashimolowo  wa kanisa la Kingsway International Christian Center anashika namba 8 huku akiwa na utajiri wa dola milioni 80 (zaidi ya shilingi bilioni 150) huku akipokea mshahara wa dola laki mbili kwa mwaka ambazo ni zaidi ya shilingi milioni 400 na mchungaji Chris Okotie wa kanisa la Household of God Church International Ministries anashika namba 9 akiwa na utajiri wa milioni 50 ambazo ni zaidi ya shilingi bilioni 100.