Tuesday, April 5, 2016

Besigye Atiwa Kizuizini tena azuiwa kuingia Kampala

 Besigye amekuwa akizuiliwa na polisi nyumbani kwake

Kiongozi wa upinzani nchini Uganda Kizza Besigye amezuiwa na maafisa wa polisi kuingia mji mkuu wa nchi hiyo Kampala.

Polisi wamemzuia alipokuwa katika makutano ya barabara za Mulago na Wandegeya karibu sana kuingia mji huo.

Wafuasi wake walikuwa wamekusanyika na polisi wametumwa kwa wingi eneo hilo.
Mwandishi wa BBC aliyeko Kampala Patience Atuhaire anasema polisi wamezuia watu kufuata gari la kiongozi huyo.

Gari ya Bw Besigye limebururwa na gari la polisi na kuelekezwa kituo cha polisi cha barabara ya Kira.

Maafisa wa polisi walikuwa wamesema Bw Besigye alikuwa na ruhusa kuingia mjini na kuhudhuria mkutano wa maombi katika makao makuu ya chama chake cha FDC kwa sharti kuwa asitatize shughuli mjini.

Bw Besigye amekuwa akizuiliwa nyumbani kwake Kisangati, viungani mwa mji wa Kampala, tangu kufanyika kwa uchaguzi mkuu nchini humo Februari.

Mkuu wa polisi Kalekezi Kayihura aliagiza maafisa wa polisi waondoke nyumbani kwa Bw Besigye Ijumaa iliyopita.