Tuesday, April 14, 2015

WATOTO 3 WALIOFUNGIWA MIAKA 10 NA MAMA YAO MWINGINE TAABANI

LILE sakata la  mama kuwafungia ndani watoto wake kwa miaka miaka 10 limechukua sura mpya baada ya mkuu wa wilaya hiyo ya Mafia kwenda Kijiji cha Kanga na kumchukua mmoja wa waliofungiwa, Muhadia Ally (pichani juu) ambaye hali yake bado ni mbaya na kumpeleka hospitali ya wilaya.
Muhadia Ally akiwa hospitali.
Habari za mama mmoja kuwafungia ndani watoto wake zimeandikwa mfululizo na gazeti hili kuanzia toleo namba 884 la Machi 31 na la Aprili 7, mwaka huu na kumshitua Mkuu wa Wilaya ya Mafia, Dk. Nassoro Hamid  aliyeamua kufunga safari hadi katika kijiji hicho akiwa ameambatana na timu maalum ya watendaji wa wilaya.
Alikuwa ameongozana na ofisa wa dawati la jinsi kutoka jeshi la polisi, ofisa ustawi wa jamii wilaya na ofisa mwandamizi kutoka ofisi ya mkurugezi wa wilaya ya Mafia ambao majina yao hayakupatikana mara moja kwa lengo la kuwachukua watoto hao na kuwapeleka hospitali.
“Nalipongeza gazeti la Uwazi kwa kufichua jambo hili na serikali itaangalia jinsi ya kuisaidia familia hii.
”Mimi mkuu wa wilaya nimepata taarifa hizi kupitia vyombo vya habari yaani gazeti lako hivyo ninapongeza kazi mliyofanya, mmefanya kwa umahiri mkubwa  bila kuchoka,” alisema mkuu huyo wa wilaya.
Muhadia Ally.
Habari ambazo zimepatikana baadaye zinadai kuwa  Mwasiti Ally ambaye ni mama wa vijana hao kumbe mwanaume aliyezaanaye, Juma Mohamed  yu hai tofauti na alivyomsimulia mwandishi wetu kwamba alifariki dunia.
“Alifanya hivyo kwa kudhani kwamba akisema hana mume angesaidiwa kwa haraka zaidi,” alisema mmoja wa majirani wa mama huyo na kwamba ni jambo walilokuwa wamepanga.Watoto waliofungiwa ndani na mama huyo ni Mzee Juma, Ally Juma aliyefariki dunia hivi karibuni na Muhadia Juma.Mkuu huyo wa wilaya alisema kwa sasa Muhadia ameanzishiwa lishe  maalumu huku akipewa kila huduma inayohitajika.