Tuesday, June 16, 2015

RAIS KIKWETE ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA WAISLAMU WOTE NA BAKWATA KUFUATIA KIFO CHA SHEIKH MKUU WA TANZANIA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais Jakaya Mrisho Kikwete ametuma salamu za rambirambi kwa Waislamu wote nchini na Baraza Kuu la Waislamu
Tanzania (BAKWATA)) kufuatia kifo cha Sheikh Mkuu wa Tanzania Mufti Sheikh Issa Bin Shaaban Simba.
Marehemu Mufti amefariki leo 15/6/2015 asubuhi katika hospitali ya TMJ – DSM alipokuwa amelazwa akisumbuliwa na ugonjwa wa sukari na shinikizo la damu (pressure).
"Kifo kinaleta huzuni, hata hivyo Kifo hakizuiliki, hatuna budi kukikubali na ni wajibu wetu kumuombea Sheikh Mkuu kwa Mola wetu ampe mapumziko ya milele". Rais Kikwete ametuma salamu hizo za rambirambi kupitia kwa Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Sheikh Alhadi Mussa Salum.
"Nawaombea subra wana familia, ndugu, jamaa, waislamu wote na wana jamii kwani Mufti alikua kiongozi katika Jamii yetu'” Rais amesema na kueleza kuwa "Kamwe mchango wake hautasahaulika katika jamii yote kwa Ujumla na hakika sote tutamkumbuka" ameongeza.
Marehemu alijiunga na BAKWATA mwaka 1968 na amekuwa mwalimu wa chuo katika mikoa mbalimbali ya Mwanza, Bukoba na Mwaka 1970 alikuwa Shekhe wa Mkoa wa Shinyanga.
Rais amemuelezea Marehemu Mufti kama mwalimu katika jamii ambaye alikua na uzoefu wa hali ya juu na mwenye kupenda dini yake na kuitumia kwa manufaa ya jamii iliyomzunguka
"Amekua mwalimu imara na mtu wa kutumainiwa na kutegemewa katika uislamu na jamii kwa ujumla, hakika
tutamkumbuka siku zote' Rais Kikwete ameongeza.
Shekhe Issa Bin Shaaban Simba alikuwa na uzoefu mkubwa ndani ya BAKWATA na aliwahi kukaimu nafasi ya
mufti kwa siku 90, baada ya kifo cha Mufti Hemed mwaka 2002.
Baada ya hapo akasimamia mchakato wa uchaguzi wa Mufti Mkuu na baadaye 2003 akachaguliwa kuwa Mufti Mkuu wa Tanzania.
Mwenyezi Mungu ailaze roho yake pahali pema Peponi, Amina.
Imetolewa na :
Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais, Msaidizi,
Ikulu-DSM
15 Juni, 2015