Thursday, July 9, 2015

RAIS KIKWETE AITAJA STARS KWENYE HOTUBA YAKE DODOMA…ATAJA SABABU ZA KUTOKWENDA UWANJANI KUISHUHUDIA

KikweteRais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Jakaya Kikwete amesema serikali yake imejitahidi katika kukuza michezo nchini Tanzania kuanzia kuajiri makocha wa kigeni na maeneo mengine ili kuleta chachu ya kukuza na kuendeleza michezo mbalimbali kwa taifa.
Kikwete amesema hayo leo wakati akilihutubia bunge mjini Dodoma, pamoja na kuzungumzia michezo mbalimbali, Rais Kikwete aliugeukia mchezo wa soka na kugusia hali ya timu ya Taifa ‘Taifa Stars’.
“Timu yetu ya Taifa haifanyi vizuri sana, tulianza vizuri, tukatumaini na mimi nikawa nakwenda pale kiwanjani navaa na jezi. Baadae wakaniambia unajua mzee ukija wewe timu hii haifanyi vizuri, nikaona hawa wanataka kusema mimi ninamkosi”, amesema Rais Kikwete.
“Nimeacha kwenda kabisa kwenye mpira, hata wakihama kutoka Dar es Salaam wakihamia Unguja tatu….kwahiyo mie siyo tatizo, tatizo wao wenyewe. Lazima watanzania tujiulize kwanini, kulikoni, hatuwezi kuendelea hivi”, ameeleza.
“Nilifanya uamuzi wa kurejesha michezo mashuleni kurejesha na mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA nia yetu ni kutaka vipaji vya vijana wetu hawa tuanze kuviibua tangu wakiwa shuleni na matumaini yetu ya usoni mambo yanaweza kuwa mazuri”, amefafanua.
Hayo ni baadhi ya maneno machache kutoka kwenye hotuba ya Mh. Rais Jakaya Kikwete wakati analihutubia bunge kwa mara ya mwisho leo mjini Dodoma wakati akieleza jitihada za serikali ambayo inamaliza muda wake madarakani.