Saturday, January 23, 2016

BREAKING NEWS: ZITTO KABWE KUBURUZWA MAHAKAMANI,IPTL WADAI ALIKUWA NA MASLAHI KWENYE TEGETA ESCROW


Wamiliki wa kampuni ya Independenti Power Tanzania Limited (IPTL) wamefungua kesi mahakamani dhidi ya mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe na mhariri wa gazeti la Raia Mwema.
IPTL wamefungua kesi pamoja na kampuni ya Pan African Power Solutions Tanzania Limited kupinga sakata la Escrow kujadiliwa tena bungeni kufuatia ripoti kadhaa walizozipata, huku wakisisitiza kuwa Zitto Kabwe alikuwa na mgongano wa maslahi wakati alipokuwa akijadili sakata la Escrow Bungeni lakini hakuweka wazi, kinyume cha kanuni za bunge na sheria kwa ujumla.
Katika maelezo yao, IPTL wameeleza kuwa kabla ya kujadiliwa kwa sakata la Escrow Bungeni, walikuwa tayari wamefungua kesi mahakani dhidi ya Zitto Kabwe na mhariri wa gazeti la Raia Mwema, wakiwashitaki kwa kusema na kuchapisha habari kwenye gazeti hilo wakidai kuwa kulikuwa na fedha za umma kwenye akaunti ya Escrow.
Wameeleza kuwa pamoja na kwamba Zitto alifahamu wazi kwamba ni kosa kushiriki kujadili bungeni kitu ambacho una mgongano wa maslahi, lakini aliendelea kushiriki mjadala uliozikandamiza kampuni hizo akiwa kama Mwenyekiti wa kamati ya PAC.
“Mheshimiwa Zitto Kabwe hakuweka wazi uwepo wa kesi hiyo sehemu yoyote katika mjadala wote wa Bunge kuhusu kile kilichoitwa ‘Sakata la Tegeta Escrow’. Kutoweka wazi huko kulipelekea Bunge kupokea taarifa au kupewa taarifa zisizo za kweli kutoka kwa mtu ambaye alikuwa na maslahi katika jambo hilo,” inasomeka sehemu ya pingamizi la IPTL.