Monday, September 14, 2015

DUUH..UNAAMBIWA HIZI NDIZO WIZARA AMBAZO MAWAZIRI WAKE WATAHITAJIKA KUFANYA KAZI USIKU NA MCHANA ENDAPO DK MAGUFULI ATAKUWA RAIS

Mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli, ameamua kuweka wazi wizara ambazo mawaziri wake watapata shida kutokana na kazi zitakazokuwa mbele yao.

Akizungumza katika mikutano midogo na mikubwa wakati akitokea Simiyu kwenda mkoani Tabora jana, Dk Magufuli, alisema mawaziri hao watapaswa kufanya kazi usiku na mchana.
 

Dk Magufuli amebainisha kuwa Waziri atakayerithi ofisi yake ya Wizara ya Ujenzi, atatakiwa kufanya kazi kuliko alivyofanya yeye na ikibidi alale katika maeneo yanayojengwa barabara.

Waziri mwingine ambaye atakuwa na kazi kubwa ni Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii ambapo Dk Magufuli amesema wizara hiyo itapaswa kuhakikisha dawa hazikosekani katika hospitali zote za umma, kuanzia zahanati katika mitaa na vijiji, vituo vya afya katika kila kata, hospitali za wilaya na hospitali za rufaa katika kila mkoa.
 

Pamoja na hayo, Dk Magufuli ameahidi wananchi kuwa katika uongozi wake, itakuwa ni mwiko kusikia mgonjwa baada ya kumuona daktari, ametumwa kwenda kununua dawa katika maduka, huku akisema kuwa waziri atakayeteuliwa kushika wizara hiyo, ajiandae kwa kuwa akishindwa ataondolewa mara moja.